1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN yajadilia mkataba wa Paris wa mabadiliko ya tabianchi

7 Novemba 2016

Mazungumzo ya Umoja wa mataifa kuhusiana na madiliko ya tabia nchi yameanza hii leo nchini, Morocco huku viongozi wakitoa wito kwa washiriki kuhakikisha makubaliano kuhusu mkataba ulioafikiwa Paris yanatekelezwa . .

https://p.dw.com/p/2SIRk
China Kohlegrupe in Shanxi
Picha: Getty Images/K. Frayer


Wajumbe kutoka mataifa 196 wanakutana nchini Morocco ambako wanajadiliana juu ya  utekelezaji wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi uliopitishwa katika mji mkuu wa Ufaransa, Paris mwezi Desemba mwaka jana.
Wakati wa ufunguzi wa kongamano hilo, waziri wa mazingira wa Ufaransa Segolene Royal alisema kuwa wamewezesha kile kilichoonekana kutowezekana na baadaye kukabidhi uongozi wa kongamano hilo kwa waziri wa mashauri ya kigeni wa Morocco Salaheddine Mezouar. 

Royal alitangaza kuwa mataifa 100 yaliidhinisha mkataba huo wa Paris uliopitishwa kuwa sheria Ijumaa iliyopita , hii ikiwa ni historia ya kutekelezwa kwa haraka kwa mkataba wa kimataifa .

Alitoa wito kwa mataifa mengine kufanya hivyo kufikia mwishoni mwa mwaka huu. 
Mazungumzo hayo ya wiki mbili mjini Marrakesh yanalenga kujadilia malengo yaliowekwa mjini Paris ambapo mataifa mbali mbali yaliwasilisha mipango binafsi ya kupunguza kiwango cha hewa inayochafua mazingira. 

Habari hizi zinajumuisha kuhakikisha mataifa yanazingatia ahadi zao za kupunguza hewa hizo na kuhakikisha dola bilioni 100 zinapatikana kila mwaka kusaidia mataifa mbali mbali kukabiliana na athari za  mabadiliko ya tabianchi.
Katika bara la Afrika ndiyo yaliokithiri mno na kwamba ni bara hili linaloathirika zaidi bila yakujali hasa kutokana na majanga yanayosababishwa na ukataji wa miti . 

Siasa za Marekani katika mkataba huo

Lakini huku wajumbe  elfu 15 wakikutana  katika mazungumzo hayo ya siku 12 huko Marrakesh, macho yote yameangaziwa nchini Marekani ambako wananchi wanapiga kura na matokeo ya uchaguzi huo yanaweza kumfanya Trump Kuwa rais mpya wa nchi hiyo-Rais Barack Obama ameshaonya kwamba linapohusu suala la viwango vya joto duniani hasara inaweza kuwa kubwa endapo Trump ataingia ikulu.  Aliongeza kusema kuwa," ufanisi wote tuliopata kuhusiana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na mkataba wa Paris ambao umechukuwa muda mrefu kuafikiwa; kilele chake kitakuwa katika kura ya hapo kesho". Alimwambia  Bill Maher, kiongozi wa kipindi cha Runinga siku ya Ijumaa. 

Mgombea  urais kwa tiketi ya chama cha Democratic HillaryClinton ameahidi  kuzingatia sera ya ndani kuhusu nishati na maazimio ya kimataifa ya mabadiliko ya tabianchi yalioafikiwa na Obama . Hata hivyo wataalamu katika kikao hicho cha Marrakesh wanasema kuwa Donald Trump hawezi kutekeleza madai yake ya kufutilia mbali mkataba huo lakini ushindi wake unaweza kurejesha nyuma ufanisi ulioafikiwa kufikia sasa. 


Mwandishi: Tatu Karema/AP/DPA
Mhariri: Yusuf Saumu