1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN kupigia kura mswada kuhusu Jerusalem

Sekione Kitojo
17 Desemba 2017

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linatafakari kupitisha mswada unaosema mabadiliko yoyote ya hadhi ya  mji wa Jerusalem hayatakuwa na athari kisheria na yanapaswa kubadilishwa.

https://p.dw.com/p/2pV23
New York UN Botschafter Ägypren Amr Abdellatif Aboulatta
Balozi wa Misri katika Umoja wa mataifa Abdellatif AboulattaPicha: picture-alliance/Zuma/L. Muzi

Misri imesambaza mswada  huo Jumamosi (16.12.2017), na wanadiplomasia  wamesema baraza  huenda  likapiga kura kuhusiana  na  mapendekezo  hayo mapema  hata  Jumatatu.

Akijitoa  katika  mwelekeo wa  kimataifa , rais  wa  Marekani Donald Trump  mwezi huu alitangaza  kwamba  atautambua  mji  wa  Jerusalem  katika  mji  mkuu  wa  Israel  na kuhamishia  ubalozi  wa  Marekani  katika  mji  huo  kutoka  Tel Aviv, hatua  hiyo  imezusha maandamano  na  shutuma  kali.

Gaza - Proteste gegen israels Militäroffensive
Maandamano ya kushutumu hatua ya Marekani kuutambua mji wa Jerusalem kuwa mji mkuu wa IsraelPicha: Getty Images

Mswada  huo  wa  azimio  uliopatikana  na  shirika  la  habari  la  AFP  unasisitiza  kwamba Jerusalem  ni  suala , "ambalo  linaamuliwa  kupitia  majadiliano"  na  kueleza "masikitiko makubwa  katika  uamuzi  wa  hivi  karibuni  kuhusiana  na  hadhi  ya  mji  wa  Jerusalem," bila kutaja  moja  kwa  moja  uamuzi  wa  rais Trump.

"Uamuzi  wowote  na  hatua  ambazo  zitaonekana  kubadilisha  hadhi, hali  na  jamii  iliyopo katika  mji  huo  mtakatifu  wa  Jerusalem  havitakuwa  na  athari  ya  kisheria, na  ni  batili  na ni  lazima  ubadilishwe," mswada  huo  umesema.

Wanadiplomasia  wanasema  wanatarajia  Marekani  kutumia  uwezo wake  wa  kura  ya turufu  kuzuwia  hatua  hiyo  wakati , wengi  kama  sio  wote , wajumbe  14  wa  baraza  la Usalama  wanatarajia  kuunga  mkono  mswada  huo  wa  azimio.

Gaza - Proteste gegen israels Militäroffensive
Maandamano Gaza kupinga hatua ya Marekani kuutambua mji wa Jerusalem kuwa mji mkuu wa Israel Picha: Getty Images

Pence kwenda Mashariki ya kati

Makamu  wa  rais  wa  Marekani  Mike Pence  atazuru  Jerusalem  siku  ya  Jumatano , akijitumbukiza   katika  mzozo  wa  moja  kati ya  suala  lenye  utata  kabisa   katika  mzozo kati  ya  Wapalestina  na  Israel.

Israel ilichukua  udhibiti  wa  sehemu  ya  mashariki  mwa  mji  huo  katika  vita  vya  mashariki ya  kati  mwaka  1967  na  inaliona  eneo  lote  la  mji  wa  Jerusalem  kuwa  mji  ambao haukugawanyika.

Mike Pence Donald Trump
Makamu wa rais wa Marekani Mike Pence Picha: picture-alliance/dpa/A.Gemignani

Wapalestina  wanaliona  eneo  la  mashariki  mwa  Jerusalem  kuwa  mji  mkuu  wao  wa hapo  baadaye.

Balozi  wa  Israel  katika  Umoja  wa  mataifa  Danny Danon "anashutumu  vikali" mswada huo , akipuuzia  kwamba  ni  juhudi za Wapalestina "kuandika  upya  historia."

"Hakuna  kura  ama  mjadala  utakaobadilisha  hali  halisi  kwamba Jerusalem ilikuwa  ama itakuwa  mji  mkuu  wa  Israel," danon  alisema  katika  taarifa.

Mswada  huo  wa  azimio  unatoa  wito kwa  nchi  zote kujizuwia  kufungua  balozi  zao   mjini Jerusalem, ukiakisi  wasi  wasi  kwamba  serikali  nyingine zinaweza  kufuata  kile  Marekani ilichofanya.

USA Trump erkennt Jerusalem als Hauptstadt Israels an
Rais Donald Trump wakati akitoa tamko la kuutambua mji wa Jerusalem kuwa mji mkuu wa IsraelPicha: Reuters/J. Ernst

Mswada  huo  unataka  kwamba  mataifa  yote  wanachama  kutotambua  hatua  yoyote ambayo  itakwenda   kinyume  na  maazimio  ya  Umoja  wa  Mataifa  kuhusu  hadhi  ya  mji huo.

Maazimio  kadhaa  ya  Umoja  wa  mataifa  yanaitaka  Israel  kujiondoa  kutoka  katika  ardhi iliyokamata  wakati  wa  vita  vya  mwaka  1967 na  kusisitiza  haja  ya  kufikisha  mwisho kulikalia  eneo  la  Wapalestina.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Isaac Gamba