Uchaguzi waahirishwa hadi mwezi ujao.
2 Januari 2008Islamabad.
Uchaguzi nchini Pakistan utaahirishwa kwa muda wa mwezi mmoja kufuatia ghasia zilizozuka kutokana na kuuwawa kwa Benazir Bhutto, licha ya vitisho vya upande wa upinzani vya kufanya maandamano mitaani hadi pale uchaguzi huo muhimu unafanyika hapo Januari 8 kama ulivyopangwa hapo awali.
Afisa mwandamizi wa tume ya uchaguzi ameliambia shirika la habari la Associated Press jana kuwa tume imekubaliana kuhusu tarehe hiyo mpya.
Amesema kuwa haitakuwa kabla ya wiki ya pili ya mwezi wa February, lakini amekataa kutamka siku kamili kabla ya tangazo rasmi leo Jumatano. Upande wa upinzani unatarajiwa kulaumu maafisa wa serikali kwa uahirishaji huo ili kukisaidia chama tawala , ambacho ni mshirika wa rais Pervez Musharaf. Msemaji wa chama cha PPP amesisitiza hata hivyo kuwa chama hicho kinataka uchaguzi ufanyike hapo Januari 8.
Zaidi ya watu 40 wameuwawa kutokana na ghasia ambazo zimezuka kufuatia kuuwawa kwa Bhutto Alhamis iliyopita.