1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Swaziland yasema waliokufa kwenye ajali ni 13 tu

1 Septemba 2015

Kinyume na taarifa zilizotolewa, serikali ya Swaziland inasema ni watu 13 tu waliopoteza maisha kwenye ajali ya barabarani iliyohusisha wanawake na wasichana waliokuwa wakielekea kwenye tamasha la densi.

https://p.dw.com/p/1GPYo
Jali ya magari Swaziland
Picha: picture alliance/AP Photo

Taarifa hiyo imeeleza kuwa wasichana na wanawake kumi, wa umri wa kati ya miaka 11 na 19 waliuawa ijumaa iliyopita, wakati lori lililokuwa likiwasafirisha wacheza densi kuelekea katika tamasha hilo la kitamaduni la kila mwaka lilipo gongana na magari mengine mawili. Wanaume watatu waliaga dunia kwenye ajali hiyo ambapo taarifa hiyo pia imetoa maelezo kuhusu umri na nyumbani anakotoka kila aliyeaga.

Mapema polisi nchini Swaziland walikataa kutoa maelezo kuhusu ajali hiyo. "Serikali inawasiliana na wazazi na familia za wahanga na wote wametambuliwa," taarifa hiyo imesema huku ikiongeza kuwa wanawake wengine watano walikuwa wangali hospitalini.

Watetezi wa haki za binaadamu wakosoa

Shirika la kutetea haki za binadamu la Swaziland Solidarity Network, limekosoa serikali kwa kutotoa idadi kamili ya walioga kwenye ajali hiyo. Shirika hilo mapema liliripoti kwamba watu 38 walikuwa wamepoteza maisha yao kwenye ajali hiyo na pia likatoa idadi zaidi na kusema idadi hiyo imefikia 65.

Mfalme Mswati III wa Swaziland
Mfalme Mswati III wa SwazilandPicha: Ishara S.KODIKARA/AFP/GettyImages

Msemaji wa shirika hilo Lucky Lukhele amesema haitakubaliwa kwamba serikali ilitumia malori yaliyowazi kuwasafirisha wacheza densi kwenda katika sherehe hizo. "Hata kama ni mmoja, mmoja ni idadi kubwa" aliongeza msemaji huyo.

Kundi hilo limemtaka mfalme wa nchi hiyo kusitisha sherehe hizo ili kuanza maombi na maombolezi ya waliofariki. Tamasha hilo la kitamaduni ambalo ni kubwa zaidi nchini Swaziland lilimalizika siku ya Jumatatu baada ya kuendelea kwa siku nane.

Huku wakivalia sketi zilizopambwa na mavazi yenye rangi mbalimbali, wasichana na wanawake hao wenye umri mdogo huwa hawafuniki matiti yao. Karibu 40,000 huimba na kucheza na pia kuleta matete yaliyomarefu kuwaliko ambayo huzuia upepo kuvuma katika makazi ya mfalme.

Namna ya kuchagua mchumba

Mfalme Mswati wa III ambaye ana wake wengi, wakati mwingine huchagua mchumba kutoka wacheza densi hao. Maelfu ya wanawake siku ya Jumatatu walicheza densi wakimuenzi mfalme huyo wa mwisho wa Afrika, mfalme Mswati wa III wa Swaziland, ambayo ni nchi changa iliyo kati ya Afrika kusini na Msumbiji.

Wasichana wakicheza ngoma katika hafla maalumu nchini Swaziland
Wasichana wakicheza ngoma katika hafla maalumu nchini SwazilandPicha: Claudine Renaud/AFP/GettyImages

Sherehe hizo za kila mwaka zinajulikana kama Umhlanga kwani wacheza densi hukata matete na kuyabeba hadi kwenye makazi ya mfalme ili kuthibiti ua la mfalme. Tarumbeta zilitangaza kushangiliwa na kuwasili kwa mfalme,akivalia ngozi ya chui na manyoya mekundu huku akizungukwa na wanaume 50 wakivalia mavazi ya kitamaduni. "Nimefurahi kumuona," amesema Prince Pinky aliyekuwa amekuja kushiriki densi kwa mara ya nne huku akisema kuwa ni furaha kuwajua wasichana wengine.

Maelfu ya wacheza densi wengine wa kati ya umri wa miaka 6 na 22 walishiriki katika densi hiyo mbele ya mama malkia. Mfalme mswati hatimaye akawakaribia wacheza densi hao huku akipita katikati yao na kuwasalimu halafu kukazuka shangwe na furaha. Wacheza densi hao amabao hujulikana kama Imbali yaani maua ,wanastahili kuwa bikira ingawa hakuna thibitisho hufanywa dhidi yao ili kubainisha.

Mfalme huyo wa mri wa miaka 47 ambaye tayari ana wanawake 14 ana hiari ya kuchagua mmoja wao kuwa mke wake. Sherehe hizo ambazo nia yake ni kuendeleza elimu ya utamaduni kwa wasichana hao na ubikira kabla ya ndoa,imeshutumiwa kwani wasichana hao huwacha sehemu zao za juu wazi na pia mavazi machache.

Wanaotetea maslahi ya wanawake wanasema sherehe hizo zinawafanya wanawake kuwa vyombo katika nchi ambayo tayari inawapa haki chache. Hlobsile Dlamini-Shongwe kutoka bunge la mashinani nchini humo amesema wasichana hao huudhuria sherehe hizo ili waonekane na kutambuliwa.

Wanawake wa Swaziland huenda wasimiliki ardhi, na wasichana wachanga wa hata umri wa miaka 13 wanaweza kuozwa kwa waume wakongwe kuwaliko ambapo mtindo huo wa kuwa na wanawake wengi huenda unasemekana kuchangia kuwepo kwa maambukizi ya juu ya virusi vya HIV huku karibu asilimia 28 ya wakazi wa kati ya miaka 15 na 49 wakiwa na virusi hivyo kulingana na shirika la Umoja wa mataifa linaloshughulika na maradhi ya ukimwi UNAIDS.

Mwandishi.Bernard Maranga/AP/DPA
Mhariri: Abdul-Rahman, Mohammed