1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Stuttgart yaparamia kileleni mwa Bundesliga

30 Aprili 2007

Baada ya Schalke ,Bremen na Bayern munich kuteleza mwishoni mwa wiki, stuttgart sasa inapigiwa upatu kuvaa taji la Ujerumani ikiwa pointi 1 tu nyuma ya viongozi wa Ligi-Schalke.

https://p.dw.com/p/CHcF

Katika changamoto iliopangwa upya ya kuania tiketi za finali ya kombe la Afrika la mataifa 2008 huko Ghana, simba wa Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo, walinguruma jana mjini Kinshasa kwa mabao 2:0 mbele ya Ethiopia.

Lomana LuaLua, alifunga safari kutoka London kwa mechi hii na kuipatia Kongo bao la penaly na kuondoka na pointi 3 kiloeoleni mwa kundi la 10.

Ilikua lakini Serge Mputu alieufumania kwanza mlango wa Ethiopia muda mfupi kabla kipindi cha mapumziko.Changamoto hii iliahirishwa mwezi uliopita baada ya mapigano kati ya vikosi vya serikali na wanamgambo wa Upinzani kusababisha vifo vya hadi watu 600 mjini Kinshasa.

Na mjini Maputo,kinyan’ganyiro cha kombe la Casle cup kilimalizika jana kwa Msumbiji kukata tiketi yake ya nusu-finali kwa kuitoa Zimbabwe katika changamoto ya mikwaju ya penalty.Timu hizo 2 zilibaki sare mwishoni mwa mchezo .

Msumbiji iliibuka kileleni mwa kundi A lililojumuisha pia Madagascar na Seryschelles.Duru 2 zaidi zimepangwa mwezi ujao na Julai na washindi wa makundi watajiunga na Msumbiji na mabingwa Zambia hapo Septemba kwa mapambano ya nusu-finali ya kombe hili la Cosafa.Kombe la castle linaaniwa na timu 13 za kusini mwa Afrika pamoja na wenyeji wa Kombe la dunia-Afrika Kusini.

Tukigeukia Ligi mashuhuri barani Ulaya, Bundesliga-Ligi ya ujerumani imezidi kupambamoto na kusisimua huku viongozi wa Ligi Schalke wako pointi 1 tu usoni huku mechi 3 tu zikisalia kumaliza msimu:

Schalke na Bremen iliopo nafasi ya pili zote mbili zilishindwa kufua dafu mwishoni mwa wiki hii wakati Stuttgart ilitamba alao kwa bao 1:0 mbele ya Borussia Mönchengladbach.

Wakati Mönchengladbach ni timu ya kwanza kuzama daraja ya pili msimu ujao, Stuttgart sasa inapigiwa upatu huenda ikaipiku Schalke na kutoroka na taji la ubingwa.Baada ya kuizamisha Mönchengladbach daraja ya pili, kocha wa Stuttgart alisema:

“Muhimu ni kushinda.Leo tumecheza kwa nidhamu kabisa na hatukufanya kile ambacho Borussia ilitazamia-yaani kuwafungulia njia ili wageuze hujuma haraka langoni mwetu.Tulionesha subira na mwishoe tuliondoka na ushindi.”

Bremen inayosimama nafasi ya tatau sasa baada ya kuzabwa mabao 2:1 na majirani zao wa kaskazini Bielefeld ya kuzabwa mabao 2:1,imeanza kama Schalke kupepesuka.Thomas Schaaf kocha wao alieleza hivi pigo walilopata jana kutoka kwa Bielefeld:

Miroslav Klose anaevumishwa atahamia Bayern munich msimu ujao,hakufua dafu katika mpambano huu na Bielefeld.Bayern Munich iliokutana na Klose , huenda ikashtakiwa kwa kufanya mkutano wa siri kumtongoza Klose kujiunga nao msimu ujao.

Kuhusu mpambano wa jana na Bielefeld Klose alisema:

“Leo tulipanga kutamba ,lakini mambo yalienda kombo.”

Katika Ligi ya Spain;FC Barcelona ilitokwa na jasho kabla mkamerun Samuel Eto’o kuipatia ushindi wa bao 1:0 dhidi ya Levante.Sevilla inasimama nafasi ya pili ya ngazi ya Ligi huko Real Madrid ikinyatia nafasi ya 3.

Huko Holland PSV Eindhoven imetwaa ubingwa wake wa 20 kwa kuongoza kwa bao 1 tu .Eindhoven imeizaba Arnhem mabao 5-1.Ajax Amsterdam iliomaliza sawa na Eindhoven zote pointi 75 iliilaza Tilburg mabao 2:0 na imelikosa taji kwa kasoro ya bao 1 tu kikapuni.

Chelsea imemudu suluhu 2:2 na Bolton Wonderers wakati Manchester imefungua mwanya wake kileleni kwa pointi 5.MANU sasa ina pointi 85 kwa 80 za Chelsea huku Liverpool ikinyatia nafasi ya 3 kwa pointi 67 baada ya kuizaba Portsmouth mabao 2-1.