1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Shinikizo dhidi ya Olmert laongezeka

Kalyango Siraj30 Mei 2008

Asema sio hongo bali 'takrima'

https://p.dw.com/p/E9hJ
Mfanyabiashara Myahudi wa Kimarekani Morris Talansky, kulia, akiwa mahakamani mjini Jerusalem Jumanne, May 27, 2008. Talansk, ni shahidi muhimu katika kesi ya hongo inayomkabili waziri mkuu wa Isreal Ehud Olmert.Picha: AP

Viongozi wa chama tawala nchini Israel cha Kadima wanapanga kukutana hivi karibuni kuamua kufanya uchaguzi wa ndani ya chama ambao unaweza kumvua madarakaka waziri mkuu Ehud Olmert kufuatia shinikizo la kumtaka kujiuzulu kutokana na madai ya kupokea hongo.

Waziri mkuu amekanusha madai ya hongo na pia hajaonyesha kuwa anampango wa kujiuzulu.

Hadi kufikia sasa waziri mkuu wa Israel-Ehud Olmert, ingawa alikiri kuwa alipokea takrima lakini amekataa kukiri kuwa alitenda makosa yoyote baada ya tajiri moja, Myahudi wa kimarekani, Morris Talansky, kukiri mbele ya mahakama mjini Jerusalem mapema wiki hii kuwa alimpa Olmert mabunda ya pesa yakiwa ndani ya bahasha.

Hata hivyo shinikizo dhidi yake linazidi kushika kasi.

Mapema wiki hii waziri wa ulinzi,Ehud Barak wa chama cha Leba, ambacho ni muhumu katika serikali ya muungano, alimtaka ajiuzulu ama aaitishe uchaguzi wa awali.

Siku moja baadae,alipata pigo jingine wakati waziri wake wa mashauri ya kigeni,Tzipi Livni,alimpa changamoto kwa kumtaka kuitisha uchaguzi mpya na kuashiria kama kiongozi huyo anafaa kung'atuka kutokana na kashfa za rushwa zinazomuandama.

Mbunge mmoja mwanamke Colette Avital alisema chama tawala ni lazima kichukue hatua za kusafisha jina lake.

Na leo ijumaa viongozi wa ngazi za juu wa chama cha Kadima ,wamesema kuwa wanapanga kukutana ili kupanga mikakati ya kufanyika uchaguzi ndani ya chama wa kutafuta kiongozi wa chama hicho.

Hata hivyo waziri mkuu amewaomba wabunge wa chama cheke hicho kutofanya chochote hadi atakaporejea kutoka safari ya mbali. Jumatatu Bw Olmert anaelekea Marekani kwa zaira rasmi ya siku tatu ambapo anatazamiwa kukutana na rais George W Bush.

Mbunge wa chama cha National Union, Arieh Eldad, hakuwa na maneno mazuri kwa waziri mkuu.Amesema kuwa waziri mkuu amenunua kazi yake kupitia njia zisizo hahali na hivyo hatua zinaf kuchukuliwa ili kulinusuru taifa la Israel.

Utafiti wa maoni nchini Israel unaonyesha kuwa kiongozi wa chama cha Likud Benjamin Netanyahu anaweza kushinda ucnaguzi mkuu ikiwa uchungizi wa rushwa utamuangusha waziri mkuu Ehud Olmert.

Uchunguzi mwingine unaonyesha kuwa waziri wa mashauri ya kigeni Tzipi Livni anawweza kushika nafasi ya pili.Livni anajipigia debe ili kumrithi Olmert kama kiongozi wa chama cha Kadima na tayari ametangaza kuwa atafanya juu chini kuona kama Olmert anaangushwa.

Hali ya sasa ya msukosuko wa kisiasa nchini Isreal ilianza kushika makali pale mfanya biashara wa kimarekani alipokiri kumpa Olmert takrima ya dola 150,000 ambazo sehemu zilitumiwa kugharimia matumizi yake ya kibinafsi.