1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Saudi Arabia yasikitishwa na kutotambuliwa Palestina

Saumu Mwasimba
19 Aprili 2024

Saudi Arabia inasema imevunjika moyo baada ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kushindwa kuidhinisha azimio la kuipatia uanachama kamili serikali ya Mamlaka ya Palestina katika Umoja huo.

https://p.dw.com/p/4exsz
Rais wa Mamlaka ya Palestina, Mahmoud Abbas.
Rais wa Mamlaka ya Palestina, Mahmoud Abbas.Picha: Ayman Nobani/dpa/picture alliance

Siku ya Alhamisi (Aprili 18), Marekani ilitumia kura yake ya turufu kuzuia hatua hiyo kuchukuliwa, licha ya kuongezeka kwa sauti za ghadhabu katika jumuiya ya kimataifa juu ya mgogoro wa kibinadamu katika Ukanda wa Gaza. 

Soma zaidi: Marekani yatumia kura ya turufu kupinga azimio la Gaza

Nchi 12 ziliunga mkono muswaada huo wa azimio uliowasilishwa katika Baraza la Umoja wa Mataifa na Algeria huku Uingereza na Uswisi zikijizuia kupiga kura.

Ofisi ya Rais Mahmoud Abbas wa Mamlaka ya Wapalestina iliitaja hatua ya Marekani kama uchokozi wa wazi unaousukuma zaidi Ukanda ya Mashariki ya Kati katika kiza.

Balozi wa Algeria katika Umoja wa Mataifa, Amar Bendjama, alisema kuungwa mkono kwa azimio hilo na wanachama wengi ni ujumbe tosha kwamba Wapalestina wanatambuliwa katika Umoja wa Mataifa.