Samaras ndiye Waziri Mkuu mpya wa Ugiriki
21 Juni 2012Gazeti linalochapishwa kila siku nchini Ugiriki la Kathimerini limesema Ugiriki, itautumia mkutano wa mawaziri wa fedha wa kanda ya sarafu ya euro, Alhamisi ijayo, kuomba mkataba huo kurefushwa kwa miaka miwili ili ipunguze nakisi ya umma hadi chini ya asilimia 3 ya pato lake la ndani.
Waziri wa fedha wa muda nchini Ugiriki Giorgos Zannias atatoa ombi hilo katika mkutano utakaoandaliwa mjini Luxembourg. Kurefushwa mkataba huo hadi mwaka wa 2016, kutautaka Umoja wa Ulaya- EU na Shirika la Fedha Ulimwenungi - IMF kutoa euro bilioni 16-20 zaidi kupitia mikopo, ikizingatiwa jinsi kiwango cha mgogoro wa kifedha kitakavyokuwa nchini humo.
Mtikisiko wa kiuchumi nchini Ugiriki umetabiriwa na EU na IMF, kuwa asilimia 4.5 ya pato jumla la ndani lakini sasa unaonekana kufikia kati ya asilimia 6 na 7. Nchi hiyo ilimaliza mkwamo wa kisiasa kwa kumwapisha kiongozi wa chama cha kihafidhina cha New Democracy Antonis Samaras Jana Jumatano kuongoza serikali ya muungano inayounga mkono mpango wa uokozi, baada ya uchaguzi uliofanyika mwishoni mwa wiki.
Samaras aliapishwa baada ya mazungumzo na washirika wake wawili wa serikali ya muungano, Kiongozi wa chama cha Kisoshalisti PASOK Evangelos Venizelos na Fotis Kouvelis wa chama cha Demovratic Left.
Idadi ya mawaziri kupunguzwa
Ripoti za vyombo vya habari zinasema serikali mpya itakuwa na mawaziri 15 na takribani manaibu 20, idadi ambayo imepunguzwa pakubwa kutoka mawaziri 49 na manaibu wao waliohudumu katika baraza la mpito la mawaziri chini ya Lucas Papademos. Kansela wa Ujerumani Angela Merkel, ambaye atahudhuria mchuano wa robo fainali wa dimba la UEFA EURO 2012 kati ya Ujerumani na Ugiriki kesho Ijumaa, amemwalika Samaras mjini Berlin kwa mazungumzo zaidi.
Ujerumani ni miongoni mwa wakopeshaji wengine wa kigeni ambao wamesisitiza kuwa wanaweza kuipa Ugiriki muda zaidi kutimiza lengo la kupunguza nakisi ambayo kwa sasa imewekwa hadi mwaka 1014 lakini hawatabadilisha kanuni halisi za mpango wa uokozi ulioafikiwa mwezi Febrauri.
Mwenyekiti wa kundi la euro jean Claude Juncker alisisitiza msimamo wa Ujerumani akisema hakuwezi kuwa na mazungumzo kuhusu kubadilisha kanuni za makubaliano ya mkataba huo, lakini jinsi ilivyosemekana wiki tatu au nne zilizopita, kwa njia yoyote ile wanaweza kuzungumza kuhusu kuurefusha mkataba huo.
Ijapokuwa alisema ataheshimu ahadi zilizotolewa na Ugiriki kwa Jumuiya ya kimataifa, Samaras alikwenda mbali zaidi katika juhudi zake, akisema atapunguza kodi ya kumiliki mali na ya mauzo na kupunguza mishahara ya watumishi wa serikali na ya malipo ya uzeeni, jambo ambalo linapingwa na wengi nchini humo
Mwandishi: Bruce Amani/DPA/AFP
Mhariri : Mohammed Abdul-rahman