1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SAINT-LOIUS : Wasenegali 102 wapotea baharini

17 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCij

Wavuvi nchini Senegal wamewaokowa wahamiaji wasio halali Wakisenegali 25 waliokuwa wakitaka kwenda Uhispania lakini wengine 102 waliokuwa kwenye boti hawajulikani walipo baharini.

Watu hao walionusurika walifikishwa kwenye hospitali ya mkoa huko Saint-Loius wakiwa wameishiwa nguvu na maji mwilini. Imeelezwa kwamba maisha ya watu hayako hatarini na kwamba wataendelea kubakia hospitalini kwa siku kadhaa kutokana na kuwa na tumbo la kuhara baada ya kumeza maji mengi mno ya chumvi katika kipindi cha siku 10 wakiwa baharini.

Baadhi ya wale walionusurika wameliambia shirika la habari la AFP kwamba kulikuweko na watu 127 kwenye boti hiyo wakati ilipofunga safari hapo Desemba 3 kutoka Bologne kusini mwa Senegal kuelekea Visiwa vya Canary vya Uhispania vilioko nje ya mwambao wa Afrika magharibi.

Hakuna habari zilizoweza kupatikana mara moja juu ya watu wengine 102 waliorepotiwa kuwemo ndani ya mashua hiyo ya mbao kadhalika iwapo kuna operesheni yoyopte ile ya kuwatafuta.