1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ROSTOCK: Ghasia zachafua maandamano dhidi ya G-8

3 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBvK

Watu 500 wamejeruhiwa na wengine 125 walikamatwa, mjini Rostock,kaskazini mwa Ujerumani baada ya machafuko kuzuka kwenye maandamano ya kupinga mkutano wa viongozi wa nchi nane tajiri G-8.Kwa mujibu wa msemaji wa polisi,wengi waliokamatwa waliachiliwa huru baada ya kuchunguza vitambulisho vyao.Polisi 430 ni miongoni mwa wale 500 waliojeruhiwa na 30 wamejeruhiwa vibaya sana. Hapo mwanzoni,maelfu ya wanaharakati waliandamana kwa amani mjini Rostock wakitoa mwito wa kulinda mazingira na kutoa misaada ya maendeleo iliyo bora zaidi.Ghasia zilizuka baada ya baadhi ya waandamanaji kuanza kuwarushia polisi mawe na mabomu ya petroli.Waziri wa ndani wa jimbo la Mecklenburg-Vorpommern,Lorenz Caffier amesema sura ya maandamano ya amani ya maelfu ya watu, imechafuliwa na mashambulizi ya kikatili yaliyotokea.Mkutano wa kilele wa kundi la nchi nane tajiri zilizoendelea kiviwanda,G-8 utafunguliwa siku ya Jumatano katika mji wa Heiligendamm ulio umbali wa kama kilomita 25 kutoka eneo la maandamano.