1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Romney ateuliwa rasmi kuwa mgombea urais kwa niaba ya chama cha Republican

Abdu Said Mtullya29 Agosti 2012

Chama cha Republican kimemteua rasmi Mit Romney kuwa mgombea urais kwa niaba ya chama hicho. Wajumbe 2061 walimpigia kura Romney kwenye mkutano mkuu uliofanyika Tampa Florida.

https://p.dw.com/p/15zEq
Mitt Romney akimbusu mkewe Ann
Mitt Romney akimbusu mkewe AnnPicha: Reuters

Mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 65 anatarajiwa kuukubali rasmi uteuzi huo katika hotuba atakayoitoa hapo kesho ambapo mkutano mkuu wa chama cha Republican unafikia kilele baada ya siku tatu .Akizungumza kwenye mkutano huo mke wa Romney Ann  aliwaambia wajumbe kwamba mumewe  hatashindwa. Aliwaabia wajumbe kwa moyo wa  uthabiti kwamba Romney ndiye mtu atakaeiinua  Marekani.

Amesema kila Mmarekani anaefikira juu ya nani anapaswa kuwa Rais ajae ajue kwamba hakuna ataekuwa na bidii  kubwa zaidi.Hakuna atakaejali zaidi na hakuna atakaefanya kila kitu kama ,Romney ili kuifanya Marekani pawe mahala bora zaidi pa kuishi

Katika hotuba yake Ann Romney alijaribu kuzigusa nyoyo za wajumbe wa chama cha Republican  na za Wamerekani wote kwa jumla alipouzungumzia upande wa mahaba wa historia ya mumewe.Alikumbusha kwamba miaka 47 iliyopita,Romney alicheza naye dansa kwa mara ya kwanza.Amesema ingawa mambo siyo mazuri wakati wote, Romney bado anaendelea kumfurahisha.Na kwa hivyo amewataka  WaMarekani wawe na imani na mumewe kwani ni mtu anaeipenda Marekani. Mama huyo amesema Romney atawapeleka  Wamarekani pazuri kama jinsi alivyompeleka yeye pazuri.    

Romney mwenyewe alipanda jukwaani na kutoa shukurani za moyo kwa wajumbe waliomteua kuwa mgombea wao katika uchaguzi wa urais ambapo  atapambana na Rais Barack Obama wa chama cha Democrats.

Katika kura za maoni za nchi nzima Romney amesimama sambamba na Rais Obama kabla ya uchaguzi utakaofanyika mnamo mwezi wa Novemba nchini Marekani. Kutokana na hali mbaya ya kiuchumi na kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu wasiokuwa na ajira nchini Marekani,huenda dau la Romney likaenda  joshi.

Hata hivyo kwa mujibu wa uchunguzi wa maoni uliofanywa hivi karibuni na Shirika la "ABC News" na gazeti la "Washington Post," Romney yupo nyuma kuhusu kukubalika. Asilimia 40 ya Wamarekani wanampa Romney nafasi ya kutegemea ushindi ,wakati asilimia 51 wamesema hana matumaini ya kushinda. 

Wajumbe kwenye mkutano mkuu wa chama  cha Republican pia walimpitisha   mbunge Paul Ryan kuwa mgombea mwenzi wa Romney katika nafasi ya Makamu  wa Rais. Ryan anazingatiwa kuwa nyota ya  chama cha Republican  inayoinukia. Wajumbe pia waliupitisha mpango wa chama unaosisitiza uongozi wa Marekani  duniani. Kulingana na mpango huo, Marekani, kwa njia ya mafumbo itazitaka nchi  za Ulaya zisipunguze bajeti zao za ulinzi. Haki ya kumiliki silaha pia inasisitizwa  katika programu  iliyopitishwa na wajumbe wa chama cha Republicana kwenye   mkutano wao mkuu unaofanyika Tampa Florida.

Mwandishi:Mtullya Abdu/Euro news/ZA/Afpe

Mhariri: Josephat Charo