1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais mteule wa Ufaransa ajiandaa kuingia madarakani

Admin.WagnerD8 Mei 2017

Rais Mteule wa Ufaransa, Emmanuel Macron, leo anaweka misingi ya kipindi cha mpito kuingia madarakani ikiwa ni pamoja na mpango wa kuizuru Ujerumani na kubadilisha jina la vuguvugu lake la kisiasa.

https://p.dw.com/p/2catd
Frankreich Hollande und Macron beim Gedenken in Paris
Picha: Getty Images/AFP/S. De Sakutin

Macron akizungumza na wafuasi wake baada ya kutangazwa mshindi wa duru ya pili ya uchaguzi wa urais nchini Ufransa uliofanyika hapo Jumapili amesema "Nitawatumikia kwa unyenyekevu, kwa nguvu. Nitawatumikia kwa ari: uhuru, usawa na umoja. Nitawatumikia kwa uaminifu na kwa imani mliyonipa, nitawatumikia kwa mapenzi. Idumu jamhuri. Idumu Ufaransa!"Macron akizungumza na wafuasi wake baada ya kutangazwa mshindi wa duru ya pili ya uchaguzi wa urais nchini Ufransa uliofanyika hapo jana.

Macron, aliyemshinda kiongozi wa sera kali za mrengo wa kulia Marine Le Pen kwa kishindo, hivi sasa lazima atafute wingi wa viti katika uchaguzi wa bunge hapo mwezi wa Juni kwa ajili ya vuguvugu lake la kisiasa lenye kama mwaka mmoja tokea kuundwa kwake.

Chama chake cha En Marche chenye kumaanisha "Kusonga Mbele" kinabadilisha jina lake wakati kikiandaa majina ya wagombea. Macron ameahidi nusu ya wagombea hao watakuwa wapya katika siasa za kuchaguliwa kama vile yeye mwenyewe binafsi alivyokuwa kabla ya uchaguzi huo wa Jumapili.

Mabadiliko makubwa kwa National Front

Frankreich Marine Le Pen nach der zweiten Runde der französischen Präsidentschaftswahlen 2017
Kiongozi wa chama cha sera kali za mrengo wa kulia Marine Le Pen.Picha: picture alliance/dpa/AP Photo/M. Euler

Chama cha sera kali za mrengo wa kulia cha National Front nacho pia kinajiandaa kubadilisha jina na kama sio kurekebisha fikra zake baada ya kushindwa vibaya kwa Le Pen.

Katika mahojiano yaliyofanyika leo hii, mkurugenzi wa kampeni wa Le Pen, David Rachline, amesema chama hicho kilichoasisiwa na baba yake kitapata jina jipya kama njia ya kuwavutia wapiga kura zaidi nchini Ufaransa.

Macron alishinda uchaguzi huo kwa asilima 66 ya kura, lakini idadi kubwa ya kura ambazo zilikuwa tupu au zilizoharibika na kujitokeza kwa idadi ndogo ya wapiga kura, jambo ambalo sio la kawaida  ni dalili ya kutoridhika kwa wapiga kura na aina ya wagombea.

Kiongozi wa sera kali za mrengo wa kulia, Marine Le Pen, ambaye alipata asilimia 35 ya kura amesema ataunda chama kipya cha kisiasa wakati uchaguzi wa bunge ukitarajiwa kufanyika hapo mwezi wa Juni.

Amesema "Chama cha National  Front ambacho kimeshiriki katika muungano wa mkakati lazima pia kibadilike sana kuweza kukidhi fursa za kihistoria na matarajio ya wananchi wa Ufaransa ambayo wameyaonyesha katika duru hii ya pili ya uchaguzi. Kwa hiyo, napendekeza kuanza mageuzi makubwa kabisa kwa vuguvugu letu ili kuwa nguvu mpya ya kisiasa ambayo Wafaransa wengi wanaitaraji na ambayo inahitajika zaidi kuliko vile ilivyokuwa hapo kabla."

Macron kuzuru Ujerumani

Frankreich Unterstützer von Emmanuel Macron feiern nach der zweiten Runde der französischen Präsidentschaftswahlen 2017
Wafuasi wa Macron wakisheherekea ushindi.Picha: picture alliance/dpa/abaca/E. Blondet

Katika kampeni yake Le Pen alitaka Ufransa ijitowe katika Umoja Ulaya na kuachana na sarafu ya euro badala yake irudi kutumia faranga ya Kifaransa.

Macron aliyelifanya suala la Umoja wa Ulaya kuwa msingi wa kampeni yake, anatarajiwa kufanya Ujerumani kuwa kituo chake cha kwanza cha ziara yake nchi za nje na pengine kuvitembelea vikosi vya Ufaransa viliko nchi za nje.

Rais huyo leo atajitokeza sambamba na Rais Francois Hollande katika maadhimisho ya kumalizika kwa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia ambayo ni siku ya mapumziko ya kitaifa yenye kuadhimisha siku ya kushindwa rasmi kwa Ujerumani katika Vita

Mwandishi: Mohamed Dahman/AP

Mhariri: Mohammed Khelef