1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Mahmoud Abbas awataka Waisrael kuondoka

Tuma Provian Dandi13 Novemba 2007

Serikali ya Palestina imesema eneo la Mashariki ya Kati linaweza kugeuka kuwa bahari ya amani na upendo ikiwa Israel itaondoka

https://p.dw.com/p/CBGw
Rais wa Israel Shimon Perez, Abdullah Gul wa Uturuki na Mahmoud Abbas wa Palestina wakiunga mikono
Rais wa Israel Shimon Perez, Abdullah Gul wa Uturuki na Mahmoud Abbas wa Palestina wakiunga mikonoPicha: AP

Rais Mahmoud Abbas amesema suluhisho la pekee linaloweza kurejesha amani katika eneo la Mashariki ya Kati ni kwa Isreal kuondoka kwenye ardhi ya Waarabu wanayoikalia kwa kipindi kirefu.

Akizungumza wakati wa mkutano uliofadhiriwa na Marekani na kufanyika mjini Ankara nchini Uturuki kwa kuzihusisha nchi za Palestina na Israel, Rais Mahmoud amesema eneo hilo litageuka kuwa bahari ya amani na upendo ikiwa Waisrael wataondoka.

Ameongeza kwa kusema kwamba watu wa eneo hilo hawataona hatari ya kupoteza maisha tena wala kujeruhiwa na kubakia na hitilafu kwenye miili yao, kwa vile muafaka utakuwa umepatikana, kilio kinachotolea na raia wa Palestina kila kukicha.

Mkutano mwingine mkubwa unatarajia kufanyika kabla ya mwisho wa mwaka huu, kwa msaada wa Marekani ambao nao una lengo la kufufua mazungumzo yaliyovunjika miaka saba iliyopita.

Baadhi ya mambo yanayoleta mvutano hadi sasa ni suala la wakimbizi wa Kipalestina, tatizo la mipaka pamoja na ufumbuzi wa mji wa Yerusalemu.

Naye Rais wa Israel Bwana Shimon Perez amesema Rais Abbas ni mpenda amani na rafiki mwema, na kwamba kwa uwepo wake akiwa mkuu wa nchi majadiliano yanaweza kufanyika na kufikia hatua nzuri.

Wakitia saini mkataba wa makubaliano kuanzisha viwanda kwenye eneo la Ukingo wa Magharibi marais hao wamesema mpango huo ni wa ushindi na kwamba unatia matumiani kwa siku za usoni.

Hata hivyo mradi huo ambao pia utatoa ajira kwa raia wengi wa Palestina utakuwa chini ya Baraza la Biashara la Uturuki, wakati jukumu la Israel litakuwa kutoa ulinzi madhubuti.

Biadhaa zitakazotengenezwa na viwanda hivyo zitapelekwa katika masoko ya Marekani, Umoja wa Ulaya na Falme za Kiarabu.