1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Raila akemea siasa za matusi Kenya

Shisia Wasilwa8 Septemba 2020

Kiongozi wa upinzani nchini Kenya Raila Odinga, amewasuta viongozi wanaowachochea wananchi kwa sababu za kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

https://p.dw.com/p/3iAem
Kenia Nairobi Opposition ehemailger Präsident Raila Odinga
Picha: Reuters/B. Ratner

Akiwahutubia waandishi wa habari alipokutana na viongozi kutoka jimbo la Kajiado, Raila alisema taifa hilo la Afrika Mashariki lina historia ya vurugu na kwamba pana haja ya kuwepo Amani wakati serikali ikikabiliana na janga la COVID 19. Hayo yanajiri huku mbunge wa eneo la Emurua Dikirr Johana Ng'eno, akishtakiwa kwa matamshi ya uchochezi.

Joto la siasa linazidi kupanda nchini Kenya kabla ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika katika kipindi cha miaka miwili ijayo. Chama tawala cha Jubilee kikionekana kuyumba, baadhi ya viongozi wanaoegemea upande wa makamu wa rais William Ruto, hawajaficha hisia zao dhidi ya kile wanachosema kuwa Ruto anadhalilishwa na bosi wake ambaye ni rais Uhuru Kenyatta.

Mpasuko huo umedhihirika kwenye baraza la mawaziri ambalo limegawanyika, huku baadhi wakionekana kumsuta Ruto. Kiongozi wa upinzani Raila Odinga, amejitosa kwenye mjadala huo, huku akiwaasa viongozi kuzingatia matamshi yao.

"Natoa wito kwa viongozi kusimamia umoja wa taifa na kuwapuuza viongozi wanaohubiri vita dhidi ya wakenya. Taifa hili lina historia ya vita kwa sababu ya siasa. Hakuna anayestahili kulirejesha taifa hili kwenye vita kwa sababu ya siasa.” Amesema Odinga..

Kwenye mtandao wake wa Twitter, Naibu wa Rais William Ruto, alikuwa mwepesi wa kuliingilia suala hilo. Ruto amewataka viongozi wanaomuunga mkono kuheshimu familia ya Rais Uhuru Kenyatta. Matamshi ya Ruto yakijiri saa chache baada ya mbunge Johanna Ng'eno kushtakiwa kwa matamshi ya uchochezi.

William Ruto ambaye ni Naibu Rais vilevile amekosoa siasa kwa kutumia matusi na lugha chafu.
William Ruto ambaye ni Naibu Rais vilevile amekosoa siasa kwa kutumia matusi na lugha chafu.Picha: Reuters/T. Mukoya

Ruto alisema kuwa matusi kwa familia ya rais sio haki ya kuhalalisha hasira. Ruto aliongeza kusema kuwa, ijapokuwa kuna tofauti katika chama, kuna njia mwafaka za kuwasilisha tofauti hizo. Junet Mohammed ni mbunge wa chama cha ODM.

"Na tunataka kummambia sasa, aache hiyo tabia mbaya ya matusi kwa serikali anayohudumu, kama anaona ametosheka atoke nje apigane akiwa nje. Tunamwambia Ruto hatuwezi kukubali siasa za vita.” Amesema Mohammed.

Kuhusu suala la BBI Raila amewahakikishia Wakenya kuwa kwa wakati mwafaka, siasa zake zitarejea, huku akipigia debe kufanyika kwa kura ya maoni kabla ya uchaguzi mkuu ujao. Raila hajatangaza nia yake ya kuwania kiti cha urais kwenye uchaguzi mkuu, japo naibu wa kiongozi wa Chama cha ODM Wycliffe Oparanya amelegeza msimamo wake na kutangaza kumuachia Raila kuwania kiti hicho kwenye uchaguzi mkuu. Hiyo ni ishara kuwa huenda Raila akawa kwenye debe katika uchaguz huo.