Polisi waendelea kupambana na waandamanaji Cairo
18 Desemba 2011Nchini Misri, kumekuwa na ghasia zaidi kati ya majeshi ya serikali na waandamanaji katikati ya mji mkuu Cairo mapema leo Jumapili katika siku ya tatu ya mapambano . Watu 10 wameuawa na 300 wamejeruhiwa kwa mujibu wa duru rasmi siku chache baada ya uchaguzi wa kwanza huru. Majeshi ya usalama yamefunga maeneo ya majengo ya serikali kwa waya.
Mashambulio ya jeshi jana Jumamosi yanafuatia ghasia kati ya waandamanaji na vikosi vya jeshi. Waziri mkuu wa mpito, Kamal al-Ganzouri, ambaye aliteuliwa na baraza la kijeshi, ametupa lawama za machafuko hayo kwa waandamanaji ambao amewashutumu kwa kulishambulia jengo la baraza la mawaziri na bunge ambapo majeshi ya usalama ilibidi wayalinde. Televisheni ya Misri imeonyesha polisi wakipambana na waandamanaji katika eneo la uwanja wa Tahrir, ikiwa ni ngome ya vuguvugu la maandamano ambalo limesababisha kuondolewa madarakani kwa rais Hosni Mubarak.