PARIS: Dominique de Villepin anahimiza vikwazo dhidi ya Iran
13 Novemba 2006Matangazo
Waziri mkuu wa Ufaransa Dominique de Villepin ametoa mwito kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuamua kwa haraka juu ya vikwazo vinavyotazamiwa kuwekwa dhidi ya Iran kuhusika na mgogoro wa kinuklia.Alipozungumza kwenye mkutano mkuu wa Wayahudi,mjini Paris,de Villepin alisema jumuiya ya kimataifa haiwezi kukubali kuiona Iran ikidhibiti silaha za kinuklia.Hadi hivi sasa hakuna makubaliano yaliopatikana kuhusu mswada wa azimio uliopendekezwa na Ufaransa,Ujerumani na Uingereza katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa sababu ya upinzani wa Urussi na China.Kwa upande mwingine,siku ya Jumapili,wizara ya mambo ya kigeni ya Iran iliarifu kuwa hadi majira ya machipuko,vyombo 3,000 vingine vitaanza kurutubisha madini ya Uranium.