1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matukio ya hivi punde kuhusu mashambulizi ya Paris

14 Novemba 2015

Maswali mengi bado yanasalia kuhusu mashambulizi ya kigaidi ya Paris ambayo yamesababisha vifo vya kiasi ya watu 128 na wengine takriban 300 wakilazwa hospitalini na majeraha.

https://p.dw.com/p/1H5sF
Picha: picture-alliance/AP Photo/C. Ena

Ni kipi kinachojulikana hadi sasa?

-Mashambulizi hayo yalifanyika jana usiku wakati washambuliaji wanane walipofanya mashambulizi katika maeneo mbali mbali katika mji mkuu wa Ufaransa, Paris

-Washambuliaji waliwafyatulia watu risasi kiholela na kuripua mabomu. Ishara zote zinaashiria yalikuwa ni mashambulizi yaliyopangwa.

-Washambulaji wanane wamekufa. Mmoja alipigiwa risasi na polisi na wengine saba walijiripua.

-Wahanga wengi wa mashambulizi hayo ni watu waliokuwa wakihudhuria tamasha ya muziki katika ukumbi wa Bataclan.

-Kulikuwa pia na mashambulizi mengine matatu yaliyolenga mikahawa na nje ya uwanja wa michezo Stade de France ambapo timu ya taifa ya Ufaransa na Ujerumani zilikuwa zinacheza.

-Rais wa Ufaransa Francois Hollande amelilaumu kundi la wanamgambo wenye itikdai kali wa dola la kiislamu IS kwa kuhusika na mashambulizi hayo

-IS imedai kuhusika katika mashambulizi hayo na kuionya Ufaransa kuwa itaishambulia iwapo itaendelea kuwashambulia nchini Syria.

- Serikali ya Ufaransa imetangza hali ya hatari, siku tatu za maombolezi, kufunga maeneo mengi ya umma na kudhibiti mipaka yake.

Ni kipi kisichojulikana?

Haijabainika wazi iwapo magaidi wote wameuawa au kama kulikuwa na washambuliaji wengine na waliowasiaidia mbali na wanane waliokufa

- Mbali na mmoja wa washambuliaji kutambuliwa kuwa raia wa Ufaransa,wengine bado haijajulikana walikuwa raia wa nchi gani au kama walikuwa wanafahamika na maafisa wa usalama kabla ya shambulizi.

- Kingine kisichojulikana mpaka sasa ni kama walitokea nchi nyingine kuja kufanya mashambulizi ama ni magaidi walio Ufaransa-

- Haijajulikana mashambulizi hayo yalipangwa lini,vipi na kama washambuliaji walijuana.

- Raia wawili wa Ubelgiji na wa Australia wametambuliwa kuwa miongoni mwa waathiriwa lakini waathiriwa wengine bado hawajatambuliwa rasmi.

Mwandishi:Caro Robi

Mhariri:Josephat Charo