1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NEW YORK : Ban kuipa kipau mbele Afrika

12 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCbb

Katibu Mkuu mpya wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema hapo jana juhudi za kuleta amani katika jimbo la Dafur nchini Sudan,Somalia na Mashariki ya Kati zitapewa kipau mbele kikubwa wakati wa ziara yake ya kwanza rasmi nchi za nje baadae mwezi huu.

Katika mkutano wake wa kwanza rasmi na waandishi wa habari tokea ashike wadhifa huo hapo Januari Mosi waziri huyo wa zamani wa mambo ya nje wa Korea Kusini ameweka wazi kwamba miongoni mwa masuala muhimu ataipa Afrika kipau mbele.

Amesema atahudhuria Mkutano wa Viongozi wa Umoja wa Afrika uliopangwa kufanyika tarehe 29 mwezi wa Januari mjini Addis Ababa Ethiopia ambapo mzozo wa Dafur na Somalia ni masuala yatakayokuwa juu kwenye agenda.

Wakati huo huo afisa mwandamizi wa serikali ya Marekani amesema hakuna mtuhumiwa yoyote yule kati ya watuhumiwa watatu wakuu wa kundi la Al Qaeda aliyeuwawa wakati wa mashambulizi ya anga ya Marekani wiki hii kusini mwa Somalia.

Afisa huyo emeongeza kusema kwamba wanajeshi wa Ethiopia wanaendelea kuwasaka watuhumiwa hao watatu kusini mwa Somalia.Mapema iliripotiwa kuuwawa kwa mwanachama mmoja mwandamizi wa Al Qaeda anayeaminiwa kuhusika na uripuaji wa mabomu katika ofisi za ubalozi wa Marekani nchini Kenya na Tanzania hapo mwaka 1998.

Afisa huyo wa serikali ya Marekani amesisitiza kwamba kulikuwa hakuna maafa ya kiraia wakati wa mashambulizi yao hayo