Netanyahu amtaka Abbas kutojitoa katika mazungumzo.
27 Septemba 2010Dakika chache tu baada ya kumalizika kwa muda wa makubaliano yaliyowekwa ya kusimamisha ujenzi wa nyumba mpya katika eneo la ukingo wa magharibi, muda ambao ulimalizika rasmi usiku wa kuamkia leo, Waziri Mkuu wa Israel ametoa ombi kwa Rais wa mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas kuendelea kushiriki katika mazungumzon ya amani, ambayo yalianza rasmi mapema mwezi huu, katika jaribio la kupatikana kwa amani kati ya Waisrael na Wapalestina.
Bwana Abbas, ambaye kwa sasa yuko ziarani nchini Ufaransa, amejibu kwa haraka ombi hilo la Netanyahu, kwa kumtaka kiongozi huyo wa Waisrael kuongeza muda wa makubaliano wa kusimamisha ujenzi huo kwa ajili ya kuyaokoa mazungumzo hayo ya amani, kama alivyofahamisha msemaji wake, Nabil Abu Rudeina.
Amesema Netanyahu lazima achukue hatua kusitisha ujenzi huo kwa ajili ya kuendelea na mchakato wa mazungumzo hayo ya amani.
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Israel, muda mfupi baada ya jua kuchomoza leo alfajiri, zana za ujenzi kama vile mabuldoza yalianza kazi katika maeneo machache ya walowezi sehemu mbalimbali za ukingo wa magharibi, ingawa si kwa kiwango kikubwa.
Aidha vimearifu kuwa ujenzi ulitarajia kuanza katika makaazi mengine manane madogo, ikiwemo katika eneo la Kiryat Arba, ambako walowezi wahafidhina takriban 600 wanaishi, eneo ambalo liko kusini mwa mji wa Hebron.
Kumalizika kwa muda huo wa makubaliano ya kusitishwa ujenzi wa makaazi ya walowezi, kuna maanisha kwamba mtu yoyote ambaye alikuwa na ruhusa ya kujenga kabla ya makubaliano hayo, kwa sasa anaweza kufanya hivyo.
Wakati mazungumzo ya amani yakiwa katika hatihati, juhudi za kimataifa bado zinaendelea kuchukuliwa, ambapo leo Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina Mahmoud Abbas ambaye bado hajaweka hadharani uamuzi wake juu ya kujitoa katika mazungumzo hayo, kutokana na ujenzi huo wa makaazi ya walowezi, anatarajiwa kukutana na Rais Nicolas Sarkozy wa Ufaransa mjini Paris kwa mazungumzo.
Bwana Abbas amewasili jana mjini Pars na kukutana na jumuia ya kiyahudi, ambapo baadaye aliwaeleza waandishi wa habari kwamba iwapo Israel haitaongeza muda wa kusitishwa kwa ujenzi wa makaazi ya walowezi, itakuwa ni kupoteza muda.
Wapalestina wanazingatia kuwa ujenzi wa makaazi ya wayahudi kama ni kikwazo kikubwa katika kupatikana kwa amani na kutishia kujitoa katika majadiliano iwapo ujenzi itaanza tena baada ya muda wa kusitishwa ujenzi huo kumalizika jana jioni.
Mwandishi: Halima Nyanza(ap,dap,afp)
Mhariri:M.Abdul-Rahman