Nchi tisa zapata pigo
14 Januari 2012Ufaransa na Austria zimeshushwa kutoka tabaka la juu kabisa na zimewekwa nafasi bora ya pili, lakini Ujerumani yenye uchumi mkubwa kabisa barani Ulaya, imenusurika. Nchi zingine za kanda ya euro kushushiwa viwango vya kuaminika kulipa madeni yake, ni Italia, Uhispania, Ureno, Cyprus, Malta, Slovakia na Slovenia.
Taarifa ya Standard & Poor´s yenye makao yake nchini Marekani imesema, imechukua hatua hiyo baada ya kukadiria sera za hivi karibuni za viongozi wa Ulaya kujaribu kuudhibiti mzozo wa fedha katika kanda ya euro. Kwa maoni ya shirika hilo, sera hizo huenda zisitoshe kuyamaliza matatizo ya kifedha katika kanda ya euro.
Agosti mwaka jana, Marekani pia, iliteremshwa kutoka tabaka la juu kabisa. Kwa sehemu fulani, mkwamo wa kisiasa ulichochea hatua hiyo na hasa kutopatikana makubaliano miongoni mwa wabunge wa Marekani juu ya njia ya kupunguza nakisi ya bajeti. Viongozi barani Ulaya, wamezihimiza serikali kupunguza matumizi na kuongeza kodi, ili kuweza kudhibiti nakisi kubwa ya bajeti. Viongozi hao wamepanga kukutana tena baadae mwezi huu, kujadili njia za kuimarisha uchumi na kuongeza ajira.
Katika mkutano wa Desemba 9, viongozi wa Umoja wa Ulaya walikubaliana kutayarisha mkataba mpya kwa azma ya kuimarisha zaidi ushirikiano wa kiuchumi, katika kanda ya euro, lakini hakuna hakika kuhusu uwezekano wa kuchukuliwa hatua zingine imara, kuumaliza mzozo wa madeni.
Mwandishi: Martin,Prema/RTRE
Mhariri: Mnette,Sudi