Mustakabali wa Westerwelle mashakani
30 Agosti 2011Wiki iliyopita, Westerwelle alizusha mabishano makali baada ya kutamka kuwa sera ya Ujerumani ya kumwekea vikwazo kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi inapaswa kusifiwa sawa na operesheni ya kijeshi ya jumuiya ya kujihami NATO. Tangu kutamka hayo,Westerwelle amekumbana na lawama kali na mito ya kumtaka ajiuzulu. Wakosoaji wanamshinikiza kukiri kuwa alifanya kosa, alipozuia kura ya Ujerumani katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa Machi 17, kuidhinisha operesheni ya kijeshi ya NATO, ili kuwalinda raia nchini Libya.
Kuna wengi wanaouliza waziwazi, mpaka lini waziri huyo atabakia na wadhifa wake. Uvumi ukienea juu ya uwezekano wa Westerwelle kujiuzulu, msemaji wa Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel amewaambia waandishi wa habari kuwa hizo ni dhana za kubuni. Amesema, kuna imani kamili kati ya Merkel na waziri wake wa nje Westerwelle. Lakini mabalozi ambao miezi hii iliyopita walikuwa wakijitahidi kutetea msimamo wa Ujerumani kuzuia kura yake, hawana uhakika.
Westerwelle alifedhehshwa pia na kiongozi mpya wa chama chake cha FDP, Philipp Roesler, alieishukuru NATO hadharani kwa kusaidia kumuonda Gaddafi madarakani. Roesler ameliambia gazeti la Rheinische Post kuwa yeye ndio alieamua kuliweka kundi la mawaziri wake katika kipindi cha majaribio. Na waziri wa nje ni miongoni mwao. Hadi mapema mwaka huu, Westerwelle alikuwa mwenyekeiti wa FDP.
Vyombo vya habari vimeshaanza kutabiri mrithi wa Westerwelle. Wengi wanaamini kuwa naibu waziri wa nje, Werner Hoyer mwenye miaka 59 ana nafasi nzuri. Yeye hana haiba lakini anaijua ndani nje wizara hiyo. Vile vile, anajuana na wanasiasa wengi wa kigeni na anaelewana na Kansela Merkel. Hata Alexander Graf Lambsdorff mwenye miaka 44 na anaekiwakilisha chama chake katika Bunge la Ulaya huenda akamrithi Westerwelle sawa na waziri wa misaada wa Ujerumani, Dirk Niebel alie na miaka 48. Wote watatu ni wanachama wa FDP. Kuambatana na kanuni za serikali ya muungano, chama cha FDP kwa sehemu kubwa kina uhuru wa kujiamulia yule atakaeshika wadhifa huo. Lakini chama hicho hakitaki kuanzisha mdahalo wa urithi, wakati majimbo mawili yakiwa na uchaguzi mwezi ujao. Lengo la chama hicho ni kushinda uchaguzi kwa sera zake za kuunga mkono makampuni na wafanyabiashara na sio, kwa sifa za watu binafsi.
Mwandishi:Martin,Prema/dpae
Mhariri:Abdul-Rahman,Mohammed