1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mume amkata mke mikono na masikio Uganda

Lubega29 Machi 2016

Kisa cha mwanamume mmoja nchini Uganda kumkata mkewe mikono na masikio kimezusha hisia mseto za hasira na huzuni kuhusu visa vya ukatili majumbani hasa dhidi ya wanawake.

https://p.dw.com/p/1ILYI
Ninsiima akiuguza najeraha katika hospitali kuu ya Mulago baada ya kukatwa na muwe wake.
Ninsiima akiuguza najeraha katika hospitali kuu ya Mulago baada ya kukatwa na muwe wake.Picha: DW/ Lubega Emmanuel

Kitendo hicho kilitokana na hatua ya mwanamke huyo Ninsiima Kabonesa ambaye kwa sasa ni mjamzito kupinga jaribio la mume wake kuuza mavuno yake ya mahindi akihisi kwamba atampunja ili hali hakuchangia chochote katika uzalishaji wake.

Chanzo cha ugomvi huo kilikuwa ni gunia 100 za mahindi aliyovuna Kabonesa kwa jasho lake mwenyewe bila mume wake kuchangia chochote. "Mwanamke huyo hukodi ardhi na kupanda zao atakalo," alisema jirani ya muathirika huyo Fatuma Nalwanga, ambaye ndiye anamhudumia kwa sasa hospitalini.

Nalwanga aliiambia DW kuwa msimu huu Kabonesa alipanda mahindi na kuvuna gunia 100. "Mume wake alijaribu kumshawishi wauze mahindi hayo Ninsiima akakataa akihisi kwamba atampunja pesa zake zote na mabishano yao yaliishia kupigana."

Ramani ya Uganda.
Ramani ya Uganda.

Vyanzo vya ukatili

Mara nyingi visa vya ukatili majumbani hutokea pale mume na mke wanapofanikiwa kuingiza mapato. Mazingira haya haya ndiyo yamempelekea Kabonesa kujikuta katika hali ya ulemavu wa milele na hali ngumu ya unyanyapaa atakamoishi akiwa mtegemezi.

Yamkini mume huyo alilenga kumuua mama watoto wake kwani alielekeza upanga aliotumia kumkata kwenye shingo. Ni katika kingakinga za Ninsiima kunusuru maisha yake ndipo alikatwa mikono na masikio.

"Mwanamke alifanya kila aliloweza kujikinga ndipo akakatwa mikono yote miwili, masikio pamoja na mgongo," alifafanua Nalwanga. Kisa hicho kimezusha hisia za hasira miongoni mwa wanaharakati wa haki za wanawake.

Polisi wanyooshewa kidole

Wakati polisi ikisema kuwa inamtafuta mume huyo, baadhi ya wanaharakati wa haki za wanawake wanahisi chombo hicho cha kisheria hakijadhihirisha jitihada hizo kwani wakati kisa hicho kilipotokea mume huyo alibaki huru hadi pale majirani wa familia hiyo walipolalamika.

"Nadhani polisi wanahitaji kufanya jitihada zaidi wamtie mbaroni mwanamume aliyemkata mikoni Niinsima. Mara nyingi washukiwa wa aina hii hawakamatwi na ndiyo maana visa hivyo vinaongezeka," alisema Tina Msuya, mkurugenzi wa kituo cha ushughulikiaji wa visa vya ukatili majumbani CEDOVIP.

Msemaji wa polisi Fred Enanga amesema jeshi hilo linamsaka bwana huyo lakini itakuwa vigumu kumpata kwani amezima simu zake zote.

Visa vya ukatili dhidi ya wanawake hutoteka mara nyingi kutokana na kipato.
Visa vya ukatili dhidi ya wanawake hutoteka mara nyingi kutokana na kipato.Picha: WeCareSolar

Kujifungua akiwa mlemavu wa kudumu

Kinachosikitisha zaidi ni kwamba katika muda wa miezi miwili hivi ijayo mama huyo mjamzito Ninsiima anataraji kujifungua na atakabiliwa na wakati mgumu kumlea mtoto wake. Hi ina maana kwamba maisha ya mtoto huyo yameathirika kabla ya kuzaliwa kwake.

"Katika muda wa miezi miwili Ninsiima hatakuwa amepona ili kumlea mtoto wake ipasavyo kisha atahitaji zaidi ya miaka miwili kujifunza jinsi ya kutumia sehemu zilizobaki za viungo vyake pamoja na kuishi katika hali hiyo ya ulemavu," alifafanua mkurugenzi wa CEDOVIP Tina Msuya.

Visa na ugomvi wa aina hii hutokea mara nyingi majumbani hasa msimu wa mavuno na wanajamii wana mtazamo kuwa pana haja kwa serikali na wadau wengine kuendesha elimu nasaha kuviepusha.

Mwandishi: Lubega Emmanuel
Mhariri: Iddi Ssessanga