1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MOSCOW: Putin asema Marekani inataka kurejesha vita baridi

28 Aprili 2007
https://p.dw.com/p/CC6M

Rais Vladmir Putin wa Urusi ameifananisha mipango ya Marekani ya kuweka makombora ya kujihami huko Ulaya ya Mashariki, na ile ya miaka ya themanini ya kuweka makombora hapa Ujerumani uliyopelekea vita baridi kati ya mataifa hayo.

Akizungumza mjini Moscow Rais Putin pia alionya mipango hiyo ya Marekani, inaongeza hatari ya kumong´onyoka kwa upendo miongoni mwa mataifa hayo.

Kiongozi huyo wa Urusi amesema hayo siku moja tu baada ya kutishia kusitisha kuwemo kwa Urusi katika mkataba wa kudhibiti silaha barani Ulaya.

Matamshi hayo ya Rais Putin yamepokelewa kwa masikitiko na Umoja wa kujihami wa Ulaya NATO.

Mkuu wa kamisheni ya Ulaya Jose Manuel Barroso alieleza kuwa tamko hilo la Rais Putin linatoa ishara mbaya, ambayo haisaidii katika kujenga mahusiano ya kidugu ambayo Ulaya inayataka na Urusi.

Mkataba huo wa kudhibiti Silaha za kawaida unaweka uwiano wa uwekaji wa ndege za kivita, vifaru na silaha nyingine ambazo hazihusiani na nuklia katika eneo la Ulaya.