Mogadishu. Uongozi mpya wa mji wa Kismayo wazuwia maandamano.
8 Oktoba 2006Viongozi wa mahakama za Kiislamu nchini Somalia wamewakamata kiasi cha watu 100 tangu siku ya Ijumaa jioni na kufyatua risasi hewani kuzuwia maandamano dhidi ya utawala mpya katika mji wa Kismayo.
Shirika la habari la AP limeripoti kuwa utawala wa mji huo unapanga kuwashughulikia wale wote waliokamatwa kwa mujibu wa sheria za Kiislamu.
Kuna habari pia kuwa muungano huo wa mahakama za Kiislamu umeamuru kufungwa kwa muda kwa mpaka wa nchi hiyo na Ethiopia, wakiyashutumu majeshi ya nchi hiyo kwa kuivamia ardhi ya Somalia.
Muungano huo wa mahakama za Kiislamu hivi sasa unadhibiti mji wa Mogadishu na sehemu kubwa ya kusini mwa Somalia , na hivi karibuni imekamata miji kadha katika bonde la Juba.
Umoja wa mataifa unasema kuwa maelfu kadha ya Wasomali wamekimbilia Kenya katika muda wa siku chache zilizopita.