MOGADISHU : Ndege ya mizigo yadunguliwa
24 Machi 2007Watu wote 11 walioko kwenye ndege ya mizigo iliodunguliwa Mogadishu hapo jana wamekufa.
Afisa wa Chama cha Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu aliekataa kutajwa jina lake amesema watu 10 wamekufa papo hapo na mmoja amefia hospitalini.
Ndege hiyo imeangukia kwenye viunga vya kaskazini mwa mji wa Mogadishu ambapo kumekuwa hakuna mapigano.
Awali wazee wa jamii ya kabila linalohodhi mji wa Mogadishu wamesema wamekubaliana kusitisha mapigano na jeshi la Ethiopia ambalo limesaidia kuiweka serikali ya mpito katika mji mkuu huo mwezi wa Desemba mwaka jana.
Zaidi ya watu 20 wameuwawa katika mapambano kati ya waasi na wanajeshi wa serikali wanaoungwa mkono na Ethiopia wakati wa mapigano ya siku mbili ambayo ni makali kabisa kuwahi kushuhudiwa kwenye mji mkuu huo mwaka huu.