1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa G20 kuanza kesho

Sekione Kitojo12 Novemba 2010

Rais Barack Obama amewasili mjini Seoul tayari kwa mkutano wa kundi la mataifa ya G20.

https://p.dw.com/p/Q5Sm
Rais Barack Obama na mkewe Michelle Obamawakiwasili mjini Seoul.Picha: AP

Rais  Barack Obama  ameamua  kugeuza  mtazamo wa mkutano  wa  G20   na   kuuelekeza  katika kuangalia  hali ambayo  haina  uwiano  sawa  duniani  na  kuziondoa  sera za  nchi  yake  katika  hali  ya  kuweza  kuchunguzwa zaidi,  wakati  huu  ambapo  viongozi  mbali  mbali  duniani wakiwasili  mjini  Seoul  kwa  ajili  ya  mkutano  wa  mataifa tajiri  na  yale  yanayoinukia  kiuchumi  ya  G20.

Taarifa  ya  mwanzo  ya  rasimu  ya   kundi  la  mataifa  ya G20   iliyodondolewa  katika   taarifa  za  soko  la  hisa  la Dow Jones, inakubaliana  na   pendekezo  la   mawaziri  wa fedha  la  hapo  kabla  la  kuwa  na  viwango  vya  thamani za  fedha   ambavyo  vinabadilika  kutokana  na  thamani ya  soko  na  haionekani  kutoa  mapendekezo  mapya  juu ya  vipi  kupunguza   hali  ya  mivutano  kati  ya  mataifa tajiri  yenye  matatizo  na  mataifa  yale  yanayoinukia kiuchumi,  kama  China  na  Brazil.

Obama  akiwa  anakabiliwa  na  shutuma  kali  kutokana na  sera  za  Marekani  za kupatikana  rahisi  fedha  wakati akiwasili  kwa  ajili  ya  mkutano  huo  wa  siku  mbili   wa viongozi  wa  kundi  la  G20 , amesema  kuwa  uchumi imara  wa  Marekani   ni  muhimu  kwa  ufufuaji  wa  uchumi wa  dunia,  na  kuwataka  viongozi   wenzake  wa G20 kuweka  kando  tofauti  zao  na  kuwajibika  ili kuimarisha ukuaji.

Iwapo  mataifa  yote  yatafanya  kile  kinachostahili  kwa upande  wao,  yale  yanayoinukia,  ama  yale yaliyoendelea, yenye   ziada,  ama  yale  ambayo  yana nakisi, sote  tutafaidika  kutokana  na  ukuaji   mkubwa, amesema  Obama  katika  barua  iliyotumwa  kwa  viongozi wa  G20 siku  ya  Jumanne.

Hatua  hiyo  ya  kuleta  maelewano  imekuja  baada   ya malumbano  makali  ya  siku  moja  wakati  wajumbe  wa majadiliano   walipokuwa  wakihangaika  kupata  taarifa  ya pamoja  ambayo  viongozi  wote  wa  G20  wanaweza  kutia saini. Mgawanyiko  mkubwa   umejitokeza  kutokana  na sera  za  kiuchumi, hususan  uamuzi  wa  Benki  kuu  ya Marekani   wiki  iliyopita  kuingiza zaidi  ya  dola  bilioni  600 katika  uchumi  wa   nchi  hiyo. Baadhi  ya  wataalamu wanaona  kuwa  hatua  hiyo huenda   ikaleta  mzozo mwingine  wa  kiuchumi  duniani.

Uchapishaji  mkubwa  wa  fedha  ama  uingizaji  wa  fedha nyingi  katika uchumi, huleta  hali  bora mwanzoni. Lakini baadaye  thamani  ya  fedha  huporomoka. Sioni  njia ambayo  inaweza  kuepusha  mfumko  wa  bei  iwapo unachapisha  fedha  kwa  wingi.

Viongozi  wa  kundi  la  G20 wana matumaini   kuwa mkutano  wa  wiki  hii utakuwa  ni  mwanzo  wa  enzi  mpya ya  ushirikiano  wa  kimataifa. Korea  ya  kusini  ambayo  ni mwenyeji  wa  mkutano  huo  imechapisha  mabango yenye  kauli  mbiu  isemayo ,  "Ukuaji  sawa  wa  kiuchumi bila  mizozo".

Mwandishi : Sekione Kitojo / rtre

Mhariri: Miraji Othman