Milio ya risasi yasikika Juba
5 Machi 2014Kwa mujibu wa mwandishi habari wa shirika la habari la Uingereza, Reuters, aliyeshuhudia mkasa huo amaesema vurugu hizo ni muendelezo wa mapigano yaliyoanza katika kipindi cha karibu miezi mitatu iliyopita ambayo yameongezka na kufikia kuwa mgogoro mkubwa.
Mwili wa mwanajeshi wa serikali ya Sudan Kusini umeonekanambele makao makuu ya jeshi, na moshi mkubwa ukifuka kutoka makao makuu hayo na kusababisha hofu kwa wakaazi na hivyo kuwafanya wakimbie ovyo mitaani.
Kauli ya mwanajeshi wa Sudan Kusini
Mwanajeshi mmoja aliekuwa akizungumza kwa sauti ya juu huku milio ya risasi ikisikika katika lango kuu la kuingilia makao makuu hayo yanayoitwa Jebel alisema "tunapambana kwa ajili ya fedha".
Katika jitihada zake ya kujenga imani kwa mtaifa wahisani, serikali ya taifa hilo jipya kabisa barani Afrika inaendesha mfumo wa malipo ambao inapaswa kufanyika ana kwa ana ili kuepusha kufanyika malipo batili kwa wafanyakazi hewa.
Mapigano haya ya sasa yameonekana kutokea kwenye kambi hiyo ya kijeshi ingawa katika kipindi kifupi majeshi ya serikali kwa kiasi kikubwa yaliwasilishwa katika mitaa iliyo karibu na kambi hiyo na kuweka vizuizi vya barabarani.
Majeshi ya kutuliza ghasia
Wakati hayo yakitokea mataifa ya Afrika yanazingatia kupeleka majeshi Sudan Kusini kwa shabaha ya kusaidia kufanikishwa utekelezaji wa kuweka silaha chini kwa pande zote hasimu yaani upande wa serikali unaoongozwa na Salva Kiir na ule wa waasi ambao kiongozi wake ni makamo wa rais wa zamani Riek Machar.
Kundi la mataifa wanachama wa pembe ya Afrika IGAD, ambalo linaendeleza mazungumzo ya upatanishi baina ya pande hizo nchini Ethiopia limesema katika taarifa yake kuwa linajadili uwezekano wa kufanikisha hatua ya kuwepo kwa jeshi la na kurejesha amani na utulivu, kwa ushirikiano wa Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa.
Hata hivyo taarifa hiyo haikuwa na ufafanuzi zaidi kuhusu kiasi au mamlaka ya jeshi hilo ingawa iliongeza kusema kuwa itakuwa kama sehemu ya chombo cha kufuatilia hali ya uhasana baina ya vikundi nchini Sudan Kusini kama ilivyokubaliwa Januari 23.
Maafisa mjini Addis Ababa wamesema mataifa ya Ethiopia, Kenya, Rwanda, na Burundi yameonesha nia ya kuchangia wanajeshi wao katika operesheni hiyo.
Maelfu ya raia wameuwawa katika mgogoro huo uliodumu kwa karibu miezi mitatu, kati ya majeshi ya serikali ya rais Salva Kiir na upande wa uasi unaongozwa na Riek Machar, ambae aliondolewa katika wadhfa wake wa umakamu wa rais mwezi Julai.
Mwandishi: Sudi Mnette/AFP/Reuters
Mhariri: Mohammed Khelef