1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Michezo mwishoni mwa wiki

13 Juni 2008

Kinyan'ganyiro cha kombe la ulaya la mataifa chaendeleo huko Uswisi na Austria,lakini pia kile cha kombe lijalo la dunia 2010.

https://p.dw.com/p/EJ6X

Baada ya changamoto za jana usiku za kufa-kupona za kombe la Ulaya kwa mabingwa wa dunia-Itali na Rumania na kati ya makamo-bingwa wa dunia - Ufaransa na Holland, leo ni zamu ya mabingwa watetezi wa Ulaya- Ugiriki kurudi uwanjani kujiokoa kuvuliwa taji na mapema. Ugiriki ina miadi leo na Russia,iliopoteza mpambano wa kwanza kwa Spian.Hii ni changamoto kati ya makocha 2 maarufu-mjerumani Otto Rehagel alieitawaza Ugiriki mabingwa wa Ulaya 23004 na Mdachi Guus Hiddink alietamba na Korea Kusini katika kombe la dunia 2002.

►◄

Kocha mjerumani wa mabingwa wa Ulaya -Ugiriki,Otto Rehagel atazamiwa sana kukibadili kikosi chake cha walinzi 5 kilichofanya madhambi pale Ugiriki ilipokomewa mabao 2:0 na Sweden.Usoni,Amanatidis anaecheza katika Bundesliga au mwenzake Nikos Liberopolous atacheza kama mshambulizi 3 .Hii ina maana hakuna nafasi leo ya kucheza kwa beki mshahara Paraskevas Antzas.

Pigo la mabao 2-1 kutoka kwa Russia, ndio mechi pekee Ugiriki ilioshindwa katika kombe la Ulaya 2004 kule Ureno kabla haikuitoa Ureno na kutoroka na kombe hadi Athens.

Katika changamoto ya pili leo, licha ya kuzabwa mabao 4-1 na Spain hapo majuzi ,kocha wa Russia-mdachi Guus Hiddink anatarajiwa kuteremsha kikosi kile kile kilichocheza mpambano wa kwanza.

Changamoto ya pili jioni hii ni kati ya Sweden na Spian.Spain iliotamba mbele ya Russia inaongozwa na kocha Luis Aragones wakati Sweden ilioikomn'goa meno Ugiriki iko chini ya uongozi wa Lars Lagerback.

Sebastian Larsson yamkinika sana leo kuchukua nafasi ya Christian Wilhelmsson alieumia.Frederick Stoor huenda nae akajaza pengo lililoachwa na Niclas Alexandersson .Kocha wa Spian Aragones huenda asikibadili kikosi chake kilichoiuma meno Russia na kuitoa kwa mabao 4-1.

Kesho jumapili,wenyeji Uswisi ambao wameshaaga mashindano wana miadi kama ada tu na Ureno inayotamba na akina christiano ronaldo.Mpambano huu unachezwa mjini Basel.

Uturuki ikiviringa ngumi kuuzingira tena mji wa Vienna, Austria kama ilivyokua katika historia ya Ottoman Empire, ina miadi na jamhuri ya Czech mjini Geneva, Uswisi.

Keshokutwa jumatatu .Hatima ya Ujerumani katika kombe hili la ulaya itajulikana baada ya juzi kuchezeshwa kwa mara ya pili kindumbwe-ndumbwe na Croatia.Ujerumani ina miadi na jirani zao Austria na ikiwa Waaustria watarudia historia yao walioiandika Cordoba,Argentina, 1978 walipoipiga kumbo Ujerumani nje ya kombe la dunia hapo 1978,Ujerumani itaaga mashindano.

Juzi kocha wa Croatia ,Slaven Bilic alikumbuka kombe la dunia 1998 huko Ufaransa alipocheza binafsi kama beki-mshahara na kuitoa Ujerumani nje ya kombe la dunia.Juzi alidai "mramba asali,harambi kweli mara moja."

Hatima ya Ujerumani kesho kutwa jumatatu kwahivyo, iko mikononi mwake.

Mbali na changamoto hizi za kombe la ulaya la mataifa-la pili kwa ukali baada ya kombe la dunia, kuna kinyan'ganyiro kinachoendelea mwishoni mwa wiki hii cha tiketi za kombe lijalo la dunia - kanda ya Afrika,Marekani ya kaskazini na kusini.Paraguay inacheza na Brazil mjini Asuncion wakati mahasimu wao Argentina wana miadi na Ecuador, mjini Buienos Aires.