1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel aitembelea Moldova

Abdu Said Mtullya22 Agosti 2012

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel anafanya ziara ya siku moja nchini Moldova kwa ajili ya kuadhimisha mwaka wa 20 wa uhusiano wa kibalozi baina ya nchi hiyo na Ujerumani

https://p.dw.com/p/15uTB
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ziarani Moldova
Kansela wa Ujerumani Merkel ziarani MoldovaPicha: Reuters

Hiyo ni ziara ya kwanza kufanywa na Kansela wa Ujerumani katika Moldova tokea nchi hiyo iwe huru baada ya kuwa chini ya himaya ya Kisoviet kwa muda wa miaka mingi. Katika ziara yake Kansela Merkel atafanya mazungumzo na mwenyeji wake Waziri Mkuu Vlad Filat , juu ya uhusiano baina ya nchi zao na juu ya masuala yanahusu Umoja wa Ulaya. Viongozi wa Ujerumani na Moldova pia wataujadili mgogoro wa sehemu ya Transnistrien. Sehemu hiyo ambayo hapo awali ilikuwa ya Moldova ilijitenga mnamo mwaka wa 1992.Merkel anatarajiwa kuziunga mkono juhudi za kuutatua mogoro huo.

Kwa muda wa miaka mingi Ujerumani imekuwa inashiriki katika juhudi za kuutatua mgogoro huo:

Msemaji wa serikali ya Ujerumani,Steffen Seibert ameeleza kwamba kwamba Ujerumani na nchi nyingine za Ulaya zitafanya juhudi ili kuitatua migogoro iliyopo katika eneo la Balkani yaani kusini-masharriki mwa Ulaya.

Mwishoni mwa mwezi wa Juni wajumbe wa Moldova na wa Transnistrien walikutana mjini Berlin kwa mara ya pili katika muda wa mwaka mmoja, kwa ajili ya mazungumzo juu ya kuutatua mgogoro wao kwa upatanishi wa Ujerumani. Miaka miwili iliyopita Kansela wa Ujerumani Angela Merkel alikubaliana na aliekuwa Rais wa Urusi Medvedev juu ya kufanya juhudi za kuutatua mgogoro wa Transnistrien.

Sehemu ya Transnistrien yenye watu wanaozungumza kirusi walijitenga na Moldova yaani sehemu ya watu wanaotumia lugha ya kiromania ,baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyomalizika mnamo mwaka wa 1992.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Berlin, ziara ya Kansela Merkel itakayochukua muda wa saa saba, ni sehemu ya juhudi za kuimarisha uhusiano baina ya Ujerumani na Moldova. Moldova iliyopo kati ya Romania na Ukraine inahesabika kuwa nchi masikini kabisa barani Ulaya.

Mwenyekiti wa jumuiya ya mawasiliano baina ya Ujerumani na Moldova,Manfred Grund amesema anayo matumaini makubwa juu ya mazungomzo ya kuutatua mgogoro baina ya Moldova na Transnistrien.Amesema anatumai hatua zitapigwa baina ya pande mbili, hizo katika masuala ya misaada ya kibinadamu,mawasiliano na ushirikiano wa kiuchumi..Hata hivyo mbunge huyo wa Ujerumani amekiri kwamba mzozo wa Moldova ni mkubwa kuliko jinsi unayoonekana kwa nje.

Mwandishi: Goncharenko,Roman

Tafsiri:Mtullya abdu.

Mhariri: Josephat Charo