Mchango kwa Ukarabati wa Chernobyl
19 Aprili 2011Umoja wa Ulaya pekee umeahidi kutoa Euro milioni 110 kusaidia kuugubika mtambo huo kwa kuta za zege. Rais wa Ukraine Viktor Yanukovych katika hotuba ya kuufungua mkutano huo mjini Kiev alisema kuwa Chernobyl ni maafa kwa dunia mzima kwa hivyo ulimwengu mzima unapaswa kushirikiana kupambana na janga hilo. Ajali ya kiwango kikubwa kama hicho haiwezi kuachiliwa Ukraine peke yake. Amesema ajali ya hivi karibuni nchini Japan pia imethibitisha kuwa matukio kama hayo ni changamoto kwa binadamu wote.
Kinu cha Chernobyl kilichomiminiwa zege hiyo miaka 25 iliyopita, sasa kina nyufa na matundu na hivyo mionzi ya sumu ya nyuklia inapenya. Ukarabati uliofanywa kati ya mwaka 2004 na 2008 umetumia vyuma kuimarisha baadhi ya kuta zilizogubika kinu hicho. Julia Marositsch anaefanya kazi katika kitengo cha ushirikiano wa kimataifa cha mtambo wa nyuklia wa Chernobyl anasema:
"Vyuma hivyo vitasaidia kuimarisha jengo hilo la zege kwa takriban miaka 15. Kwa hivyo kuna muda wa kufanya ukarabati na kumimina zege jipya ili kuwa na kuta imara zaidi."
Kazi hiyo ya ukarabati inahitaji muda huo, kwani kazi ya mradi huo mkubwa ni ngumu kuliko vile ilivyotazamiwa kama anavyoeleza Heinz Smital, mtaalamu wa kinga ya mionzi ya nyuklia wa shirika la ulinzi wa mazingira Greenpeace.
"Haiwezekani kufanya kazi juu ya jengo hilo kwani katika sehemu hiyo viwango vya mionzi ya nyuklia ni vikubwa mno."
Gharama za ukarabati zinaongezeka kila mwaka. Kwa hivi sasa, inatathminiwa kuwa kutahitajiwa kiasi cha Euro bilioni 1 nukta 6 - na jumuiya ya kimataifa inatoa msaada - mfadhili mkubwa ni Umoja wa Ulaya. Na msaada huo unahitajiwa, kwani bado kuna hatari kubwa. Inatathminiwa kuwa asilimia 5 tu ya mionzi ya nyuklia ndio iliyotawanyika wakati wa mripuko. Hiyo humaanisha asilimia 95 bado zimo ndani ya mtambo huo. Na taka hizo za nyuklia lazima zizuiliwe ndani kwa njia yo yote ile anasema Heinz Smital wa Greenpeace.
Mwandishi:Nagel,Christina/ZPR/P.Martin
Mhariri:Abdul-Rahman,Mohammed