1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya kujadili vita vya Gaza kufanyika Saudi Arabia

26 Aprili 2024

Viongozi kutoka nchi za Kiarabu na Ulaya watakutana siku ya Jumapili nchini Saudi Arabia katika mkutano wa kilele wa kiuchumi pamoja na mazungumzo ya Jumatatu yatakayojadili vita vya Gaza.

https://p.dw.com/p/4fEgr
Saudi Arabia | Mkutano wa Viongozi wa nchi za kiarabu mjini Riyadh
Picha ya pamoja ya viongozi wa mataifa ya kiarabu walipokutana mjini Riyadh, Saudi Arabia kujadili vita vinavyoendelea huko Gaza: 11.11.2023Picha: WANA NEWS AGENCY/REUTERS

Wanadiplomasia wakuu wa nchi za  Kiarabu na Ulaya wanatarajiwa kuanza kuwasili katika mji mkuu wa Saudi Arabia, Riyadh, mwishoni mwa wiki hii kushiriki mkutano wa kilele wa kiuchumi pamoja na mikutano kuhusu vita huko Gaza.    

Mkutano huo maalum wa siku mbili wa Jukwaa la Kiuchumi la Dunia, umepangwa kuanza siku ya Jumapili, na utawajumuisha miongoni mwa viongozi wengine, mawaziri wa mambo ya nje wa Saudia, Jordan, Misri na Uturuki.

Soma zaidi:Mataifa ya kiisalam yaikosoa Marekani katika vita ya Gaza

Siku ya Jumatatu, kutafanyika kikao kitakachoangazia vita vya Gaza na kinatarajiwa kumshirikisha Waziri Mkuu mteule wa Palestina Mohammed Mustafa, Waziri Mkuu wa Misri Mostafa Madbouly na Sigrid Kaag, mratibu wa misaada wa Umoja wa Mataifa huko Gaza. Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa Stephane Sejourné ni miongoni mwa maafisa wa Ulaya watakaosafiri kuelekea  Saudi Arabia  kuhudhuria mkutano huo.

Misri yatuma ujumbe huko Israel

Ujumbe huo wa ngazi ya juu kutoka Misri na unaoongozwa na afisa mkuu wa upelelezi wa Misri, Abbas Kamel, unalenga kujadili na Israel kuhusu mipango ya usitishwaji mapigano kwa muda mrefu huko Gaza. Wakati huo huo, serikali mjini Cairo imeonya kuwa mashambulizi ya Israel katika mji wa Rafah unaopakana na Misri, yatakuwa na athari kubwa kwa  utulivu wa kikanda.

Wakati vita vikiendelea kupamba moto huku idadi ya vifo na majeruhi vikiongezeka, shinikizo la kimataifa pia limeongezeka la kuzitaka  Israel na kundi la Hamas  wafikie makubaliano ya kusitisha mapigano.

Jordan | Maandamano ya kuwaunga mkono wa Palestina
Raia wa Jordan wakiandamana kuwaunga mkono Wapalestina kufuatia vita vinavyoendelea Gaza: 05.04.2024Picha: Alaa Al Sukhni/REUTERS

Raia wa Jordan waliandamana leo baada ya sala ya Ijumaa kuwaunga mkono Wapalestina. Qassem Al-Kubaai ni mmoja wao:

"Baada ya siku 200 za mashambulizi, baada ya mashahidi elfu 34,000 kuuawa, baada ya laki moja ya wengine kujeruhiwa na kusalia chini ya vifusi, baada ya kubomolewa kwa shule na hospitali, na baada ya yote hayo, ni wakati sasa wa serikali na nchi za Kiarabu kuchukua hatua."

Soma pia: Viongozi wa mataifa ya kiarabu na kiislamu wataka kukomeshwa vita vya Gaza

Afisa wa Misri amesema kwa sharti la kutotajwa jina kuwa mazungumzo ya leo huko Tel-Aviv yatalenga kwanza juu ya ubadilishanaji wa mateka wanaoshikiliwa na Hamas pamoja na wafungwa wa Kipalestina wanaoshikiliwa katika magereza ya Israel. Kutajadiliwa pia suala la kurejeshwa kwa idadi kubwa ya Wapalestina waliokimbia makazi yao kaskazini mwa Gaza.

(Vyanzo: Mashirika)