1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

May kuhimiza viongozi wa EU kupitisha makubaliano ya Brexit

Sylvia Mwehozi
14 Desemba 2017

Waziri mkuu wa Uingereza Theresa May anaelekea mjini Brussels hii leo ambapo atawahimiza viongozi wa Umoja wa Ulaya kuidhinisha makubaliano ya kusogeza mbele mazungumzo ya Brexit katika awamu ya pili.

https://p.dw.com/p/2pLsN
Frankreich - One Planet Summit - Theresa May
Picha: Reuters/B. Tessier

Waziri mkuu wa Uingereza Theresa May anaelekea mjini Brussels hii leo ambapo atawahimiza viongozi wa Umoja wa Ulaya kuidhinisha makubaliano ya kusogeza mbele mazungumzo ya Brexit katika awamu ya pili, akieleza kuwa ni mpango wa haki unaotoa msingi mzuri wa majadiliano ya mahusiano ya baadae. 

Mwanzoni mwa chakula cha jioni mjini Brussels, saa 24 baada ya matokeo ya kushangaza ya bunge nyumbani, waziri mkuu May atarudia hoja yake ya kufungua mazungumzo ya kufumua zaidi ya miaka 40 ya muungano ili kuruhusu majadiliano ya biashara ya baadae, ambayo anaona kama ni muhimu katika kutoa uhakika wa biashara.

Viongozi wengine 27 wa Umoja huo wote lakini wana uhakika wa kuthibitisha mpango wa kusonga mbele katika awamu ya pili siku ya kesho Ijumaa, baada ya May kuondoka mjini Brussels, akianzisha hatua nyingine ya mazungumzo yanayoweza kuzuiwa na mgawanyiko nyumbani na tofauti ndani ya Umoja wa Ulaya.

England Parlament stimmt über Brexit ab
Bunge la Uingereza katika mjadala mkali wa BrexitPicha: picture alliance/dpa/AP Photo

Kura ya bunge 

Katika pigo lingine kwa May, ambaye tayari amedhoofika baada ya kupoteza wingi wa viti katika chama cha Conservative kwenye uchaguzi wa Juni, bunge hapo jana limepiga kura ya marekebisho ambayo yanahitaji kura ya maana ya bunge hapo baadae juu ya mpango wowote wa mwisho wa Brexit. Hadi dakika ya mwisho ya mjadala mgumu, timu ya May ilijaribu kuwashawishi wabunge katika chama chake ili kuzuia hoja hiyo, ambayo serikali inaona kwamba itadhoofisha mkono wake katika majadiliano ya Brexit. Lakini wabunge wa kutosha wa Conservative waliasi na kushinda kwa kura 309 kuunga mkono mabadiliko ili kulipa bunge mamlaka ya kuamua juu ya Brexit na wabunge 305 waliyapinga mabadiliko hayo.

Baada ya kura hiyo, kiongozi wa chama cha Labour Jeremy Corbyn amesema kwamba, "Hatimaye bunge limefany akazi yake. Waziri mkuu alijaribu kunyakua madaraka kwa nguvu, akijaribu kushinikiza muswada wa Umoja wa Ulaya bila ya kuzingatia bunge na kuchukua madaraka ya bunge, bunge limekataa na kushinda kura ambayo inasema lazima kuwepo na uamuzi sahihi wa bunge la Uingereza juu yamasharti na kitakachotokea juu ya majadiliano ya Brexit." 

Mafanikio ya May 

Baada ya siku kadhaa za diplomasia, May aliweza kuokoa mpango wa mwisho Ijumaa iliyopita, na kutuliza wasiwasi wa mshirika wake Ireland ya Kaskazini juu ya kulinda uhuru wa mpaka na mwanachama wa Umoja wa Ulaya Ireland bila ya kutenga jimbo hilo kutoka Uingereza.

Großbritannien Labour Chef Jeremy Corbyn
Kiongozi wa chama cha Labour nchini Uingereza, Jeremy CorbynPicha: Getty Images/AFP/L. Parnaby

Kisha, wazungumzaji wakuu wa Umoja wa Ulaya walisema kwamba mazungumzo yamepiga hatua muhimu, pendekezo ambalo, litazuia ajali na kubarikiwa na viongozi wengine wanachama wa umoja huo. Mafanikio yake yamempatia nafasi ya kupumua nyumbani kisiasa baina ya wanaounga mkono na walio na wasiwasi kuhusu Brexit ndani ya chama chake, na yamepunguza matarajio ya machafuko kutokana na kuondoka katika Umoja huo.

Lakini kuna vikwazo bado vinakuja. May na baraza lake Jumanne ijayo watakuwa na mazungumzo na mawaziri wandamizi walio na mawazo shindani juu ya mustakabali wa baadae nje ya Umoja huo, ikiwa ni kubakia karibu na umoja huo au kuanzisha mpango mpya.

Umoja huo uko tayari kuanza mazungumzo mwezi ujao kwa kipindi cha miaka miwili ya mpito ili kuondoa wasiwasi wa Uingereza baada ya Machi 2019, lakini unataka maelezo ya kina kutoka London juu ya nini inataka kabla haijafungua majadiliano ya biashara kuanzia mwezi wa Machi.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/Reuters

Mhariri: Saumu Mwasimba