Mashindano ya kombe la mataifa ya Afrika yapamba moto
22 Januari 2012Katika muda wa wiki tatu zijazo , nyota wa soka kama Didier Drogba wa Chelsea ya Uingereza na Yaya Toure wa Manchester City wataonyesha umahiri wao katika mashindano makuu katika bara la Afrika yanayofanyika nchini Gabon na Guinea ya Ikweta.
Kwa taifa hilo dogo la Afrika ya kati la Guinea ya Ikweta , ambalo ni mwenyeji mwenza wa kombe hilo la mataifa ya Afrika pamoja na Gabon ni nafasi yake ya kujionyesha duniani kuhusu maendele ya haraka yanayopigwa baada ya kiasi cha muongo mmoja tu wa maendeleo yanayopewa nguvu na nchi hiyo kuwa msafirishaji wa mafuta.
Hata hivyo tamasha hilo la soka linafunika baadhi ya matatizo yaliyojificha. Nchi hiyo inajikuta katika ukweli wa machungu wa ukandamizaji pamoja na umasikini uliokithiri, amesema Daniel Bekele, mkurugenzi wa shirika la Human Rights Watch katika bara la Afrika , ambaye anaamini kuwa hali bora ya maendeleo nchini humo yanafunika picha halisi inayowakabili watu masikini wa Guinea ya Ikweta.
Ushahidi wa maendeleo hayo unaonekana kila mahali, ambao ulioanzishwa na ugunduzi wa mafuta mwaka 1994. Ndege zinazowasili katika mji mkuu Malabo zinaruka juu ya eneo linalokuwa kwa kasi upande wa pwani, ikiwa ni ushahidi wa zaidi ya mapipa 300,000 yanayozalisha kila siku nchini humo. Mafuta mengi yanapelekwa nchini Marekani.
Demokrasia ni moja kati ya mambo ambayo wananchi wa Guinea ya Ikweta wanakosa, kwa mujibu wa wachunguzi wa kimataifa.
Rais Teodoro Obiang Nguema Mbasongo ameitawala nchi hiyo tangu mwaka 1979, wakati alipochukua madaraka katika mapinduzi na utawala wake unaonekana kuwa miongoni mwa tawala kandamizaji kabisa katika bara la Afrika.
Mbali na hali hii, tamasha kubwa kabisa la soka katika bara la Afrika lilianza siku ya Jumamosi katika mji wa bandari wa Bata, mji wa kibiashara wa nchi hiyo. Timu ya Guinea ya Ikweta , ambayo inaonekana kuwa katika kiwango cha chini kabisa , ilifanya maajabu kwa kuishinda Libya kwa bao 1-0 katika mchezo wa ufunguzi.
Upande wa pili wa viwango vya soka katika bara la Afrika , tukio hilo pia lina vigogo wa soka kama Cote D'Ivore, ambayo inacheza katika mji wa Malabo, na nyota wake wengi ambao wanalipwa fedha nyingi katika timu za soka za Ulaya , kama Drogba na ndugu wawili Yaya na Kolo Toure.
Jumatatu itakuwa zamu ya Morocco na Tunisia kuonyesha kazi na kisha Gabon wenyeji wa mashindano hayo wataonyeshana kazi na Niger.