Netany<ahu awaudhi washirika wake
8 Oktoba 2015Uamuzi wa Benjamin Netanyahu anaetaka kujaribu kutuliza hali ya mambo,unamtia katika hali ya mfarakano pamoja na wafuasi wa itikadi kali ndani ya serikali yake ya muungano.Wao ndio waliokuwa wakimshinikiza waziri mkuu Netanyahu apitishe hatua kali kukomesha matumizi ya nguvu pamoja na kuzidisha harakati za ujenzi wa makaazi mepya ya wahamiaji wa kiyahudi.
Lakini Netanyahu anahofia pia asije akawaudhi viongozi wa serikali ya Marekani pamoja na kukabiliwa na wimbi jengine la ghadhabu za wapalastina, Intifadha ambalo madhara yake yangekuwa makubwa kwa pande zote mbili-Israel na Palastina.
Israel inakanusha madai inataka kulikalia eneo la Harami Sharif
Eneo la mlima-Harami Sharif ndio kitovu cha mzozo huu wa sasa.Waislaam wanalitukuza eneo hilo kuwa ni mahala ambako Mtume Muhammad alipanda mbinguni huku mayahudi kwa upande wao wakiliangalia kama eneo yanakokutikana mahekalu mawili ya kale ya kiyahudi.
Wapalastina wengi wanaamini Israel inajaribu kueneza ushawishi wa kiyahudi katika eneo hilo,madai ambayo Israel daima imekuwa ikiyakanusha.
Waziri mkuu wa Israel Netanyahu ameamuru marufuku kwa mawaziri wake na wabunge wa Israel kulitembelea eneo hilo kwasababu ya hofu ziara hizo zinaweza kuzidisha matumizi ya nguvu-hayo lakini ni kwa mujibu wa afisa mmoja wa serikali ya Israel ambae hakutaka jina lake litajwe.
Mwaka 2000 kiongozi wa wakati ule wa upinzani Ariel Sharon alilitembelea eneo hilo na kupelekea kuripuka wimbi la pili la ghadhabu za wapalastina Intifadha.
Wabunge wa kiarabu wanasema wataingia katika msikiti wa Al Aqsa
Amri hii mpya ya Netanyahu imewaudhi washirika wake serikalini;Waziri wa kilimo,Uri Ariel wa chama kinachowaunga mkono walowezi wa kiyahudi ambae hivi karibuni alilitembelea eneo hilo amesema hivi punde atalizungumzia suala hilo moja kwa kwa moja na Netanyahu.
Wabunge wa kiarabu nao pia wanabisha uamuzi huo.Wanasema hakuna,"si Netanyahu na wala si mrengo wa kulia atakaewazuwia kuingia katika msikiti wao wa Al Aqsa"."Uamuzi wa Netanyahu hauna maana na ni kinyume na sheria" amesema mbunge wa kiarabu wa Israel Ahmad Tibi katika taarifa yake akiahidi kesho ijumaa wote watakwenda kusali katika Msikiti wa Al Aqsa unaokutikana kafika eneo hilo la Harami-Sharif au Mlima wa Mahekalu kama wanavyoliita wayahudi.Itafaa kusema hapa kwamba kati ya wabunge 120 wa bunge la Israel-Knesset,13 ni waarabu.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/dpa/AP
Mhariri: Iddi Ssessanga