1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani kutambua Jerusalem kuwa mji mkuu Israel

Oumilkheir Hamidou
6 Desemba 2017

Rais Donald Trump wa Marekani anatarajiwa kutangaza kwamba Marekani inaitambua Jerusalem kuwa mji mkuu wa Israel na itauhamishia ubalozi wake mjini humo

https://p.dw.com/p/2osaq
Palästina Gaza Proteste
Picha: Reuters/M. Salem

Licha ya maonyo kutoka nchin za Magharibi na washirika wa nchi za Kiarabu, Donald Trump anapanga kutoa hotuba yake akiwa ikulu ya White House, saa moja za usiku kwa saa za Ulaya ya Kati kuiamuru wizara ya mambo ya nchi za nje ianze kutafuta mahala utakapohamishiwa ubalozi wa Marekani mjini Jerusalem, ikiwa ni sehemu ya kile kinachotarajiwa kuwa utaratibu wa muda mrefu wa kuhama ubalozi huo kutoka Tel Aviv.

Kanuni za mji wa Jerusalem ni mojawapo ya pingamizi kubwa katika juhudi za miongo kadhaa za kusaka ufumbuzi wa amani wa mzozo kati ya Israel na Palestina. Israel inauangalia mji huo kuwa ni mji wao wa milele na usiogawika na inataka balozi zote zihamishiwe huko. Wapalestina lakini wanataka eneo la mashariki la Jerusalem liwe mji mkuu wa dola huru la Palestina.

Washirika wa Washington katika  Mashariki ya Kati wameonya dhidi ya balaa linaloweza kusababishwa na uamuzi wa Rais Trump.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki ulimwenguni, Papa Francis, ametoa wito wa kuheshimiwa kanuni zilizopo za mji wa Jerusalem na kusema mivutano ziada katika eneo la Mashariki ya Kati itazidisha makali ya mizozo ulimwenguni. China na Urusi zimeelezea wasiwasi zikisema mipango ya Marekani inaweza kuzidisha makali ya uhasama katika eneo la Mashariki ya Kati.

Israel US Botschaft in Tel Aviv
Marekani itauhamisha ubalozi wake kutoka Tel vivPicha: Getty Images/AFP/J. Guez

Trump anasema atatia saini waraka kuchelewesha hatua hiyo kwa kuwa mjini Jerusalem hakuna mahala ambako ubalozi wa Marekani unaweza kuhamishiwa. Afisa wa ngazi ya juu wa Marekani amesema patahitajika kati ya miaka mitatu na minne hadi ubalozi huo utakapofunguliwa mjini Jerusalem.

Lakini uamuzi wa Trump, unaotokana na ahadi aliyotoa katika kampeni nzake za uchaguzi mwaka jana, utaipindua sera ya jadi ya Marekani inayoiangalia kanuni ya Jerusalem kama ni sehemu ya ufumbuzi wa mataifa mawili, Israel na Palestina.

Wapalestina wanasema uamuzi wa Trump utamaanisha mwisho wa ufumbuzi wa mataifa mawili. "Anatangaza vita mashariki ya kati, anatangaza vita dhidi ya Waislamu bilioni moja na nusu na mamia kwa mamilioni ya Wakristo ambao hawatokubali maeneo yao matukufu yawe chini ya usimamizi wa Israel." Amesema hayo Manuel Hassassian ambae ni mwakilishi mkuu wa Wapalestina nchini Uingereza.

Waziri Mkuu Theresa May anapanga kumpigia simu Rais Trump kuhusu dhamira yake hiyo. Akizungumza bungeni hii leo, waziri mkuu huyo wa Uingereza amesema msimamo wao haujabadilika na kwamba kanuni za mji wa Jerusalem zinabidi ziamuliwe kwaa njia ya mazungumzo kati ya Israel na Palastina na kwamba Jerusalem uwe mji mkuu wao wa pamoja.

Kwa upande wake, Rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa mazungumzo yake pamoja na Mfalme Abdallah wa Pili wa Jordan wametilia mkazo Jerusalem ya Mashariki ndio mji mkuu wa taifa la siku za mbele la Palestina. Jumuia ya nchi za kiarabu itakutana jumamosi inasokuja akuzungumzia uamuzi wa Donald Trump.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Reuters/AFP
Mhariri: Mohammed Khelef