1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wajerumani waadhimisha siku ya Muungano

3 Oktoba 2017

Siku kuu ya Muungano inaadhimishwa safari hii baada ya uchaguzi mkuu katika wakati ambapo wajerumani wanatafakari. mnamo wakati ambapo nchi yaao inabidi iwajibike kimataifa

https://p.dw.com/p/2l8Rp
Deutsche Einheit
Picha: picture-alliance/dpa

Wajerumani wanaadhimisha miaka 27 hii leo tangu walipoungana upya baada ya kuporomoshwa ukuta wa Berlin . Mhariri mkuu wa DW Ines Pohl anasema katika uhariri wake licha ya baadhi ya shida zilizopo, matarajio ambayo bado hayakukamilika na miradi ambayo haikutekelezwa, siku ya leo ni siku ya furaha.

Oktoba tatu ni siku ambayo ulimwengu mzima unaikodolea macho kwa fahari nchi hii ambayo licha ya kubeba jukumu la maovu kadhaa, imefanikiwa kuuvunja kwa amani ukuta uliokuwa ukiigawa kwa mda mrefu na kuungana upya ikiwa nchi ya kidemokrasi inayoaminika na inayonawiri kiuchumi, nchi inayoelekea kuwa mhimili mmojawapo kati ya mihimili ya ulimwengu wa magharibi.

Lakini baadae ukaitishwa uchaguzi mkuu mwaka 2017. Na chama cha siasa kali za mrengo wa kulia, Chaguo Mbadala kwa Ujerumani-AfD kikajipatia karibu asili mia 13 ya kura na kugeuka nguvu ya tatu ya kisiasa.Tangu wakati huo, kauli mbiu ya wakaazi wa Jamhuri ya kidemokrasi ya Ujerumani ya zamani au GDR ya kudai uhuru ikabadilika."Sisi ndio wananchi" ndio kauli iliyokuwa ikihanikiza Dresden na katika miji mengine mnamo mwaka 1989 na kupelekea kuporomoka mfumo wa kimabavu wa GDR."Sisi ndio wananchi" inamaanisha tunataka demokrasia katika nchi tunayoishi.

Mhariri mkuu wa DW, Ines Pohl
Mhariri mkuu wa DW, Ines PohlPicha: DW/P. Böll

Kauli mbiu "Sisi ndio Wananchi "inatumiwa vibaya

Hii leo, baada ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia, AfD, kufanikiwa kwa mara ya kwanza kuwakilishwa katika bunge la shirikisho Bundestag, kauli mbiu hiyo inasikika vyengine kabisa. Katika kauli hii "Sisi ndio Wananchi" kinachopewa umuhimu sio tena madai ya kuwa na mfumo wa kidemokrasia. Kwa wengi ujumbe mkuu wa kauli hiyo umegeuka kuwa "Sisi ndio Wananchi" na sio nyie. Nyie hammo na huku siko kabisa. Ujumbe huo unawalenga wakimbizi walioingia Ujerumani miaka miwili iliyopita ili kutafuta kinga na mustakbali mwema wa maisha. Lakini pia ni jibu kwa ulimwengu uliopoteza dira ambako hakuna kilichokuwepo kilichoko au kitakachokuwa kama kilivyokuwa.

Mamilioni ya watu wameingia njiani kwasababu makwao hawawezi au hawataki tena kuishi, kwasababu wametimuliwa na  vita, maradhi ya kuambukiza, ukame na mafuriko. Mamilioni wengine watafuata. Hawatokubali kuzuwiliwa kwa urahisi, wanataka na wao pia wapatiwe haki ya kuwa na maisha bora ya kupigania maisha bora. Watu hao hawatokimbilia wote ulaya. Vuguvugu la wakimbizi na matokeo yake lakini yatashuhudiwa katika kila pembe ya dunia.

Ndio maana kauli hii ya "Sisi ndio Wananchi" sio kilio cha wasiojua la kufanya, kilicholengwa kwa wanasiasa, bali pia kilio cha asili mia 87 ya wapiga kura wa Ujerumani wanaowapinga AfD. Kinyume na mwaka 1989, waliopaza sauti "sisi ndio Wananchi" hawakuwa wananchi walio wengi.

Shereha za Octoba tatu zinachukua sura ya kuwajibika na sio tu kutafakari

Na licha ya hayo, kuendelea kana kwamba hakuna kilichotokea sio jibu la kishsindo cha uchaguzi mkuu. Hata majadilianao tete ya kuunda serikali ya muungano ni ushahidi wa suala linalobidi kupatiwa jibu nalo ni jee tunataka kuishi katika nchi ya aina gani? Muhimu kwasasa ni kupigania kuwa na Ujerumani inayojitambulisha kuwa mwanachama kamili wa Umoja wa ulaya , nchi inayofuata mwongozo wa sheria msingi na kuutumia utajiri wake pia  katika kuwasaidia wale wanaohitaji kusaidiwa. Ujerumani inasherehekea siku ya Muungano. Ni sherehe ambayo kwa mwaka huu wa 2017 inachukua sura ya waajib badala ya kutafakari tu.

 

Mwandishi: Pohl Ines/Hamidou Oummilkheir

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman