1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaVatican

Makundi mawili ya wapiganaji yafanya mashambulizi Urusi

Tatu Karema
12 Machi 2024

Makundi mawili ya wapiganaji wenye silaha yenye makao yake nchini Ukraine na yanayodaiwa kuundwa na raia wa Urusi wanaopinga vita vya nchi yao nchini Ukraine, yamefanya uvamizi katika mpaka wa Magharibi wa Urusi

https://p.dw.com/p/4dQ5b
Wanajeshi wa Ukraine wakipata mafunzo katika eneo la Donetsk mnamo Novemba 2023
Wanajeshi wa Ukraine Picha: Hanna Sokolova-Stekh/DW

Kupitia kurasa zao za mtandao wa kijamii wa Telegram, kundi la wapiganaji wanaopinga vita vya Urusi dhidi ya Ukraine na kikosi cha wapiganaji wa Siberia yametangaza kwamba yamefanya mashambulizi kutoka Ukraine kuelekea Urusi.

Kundi hilo linalopinga vita vya Urusi, limeongeza kuwa watachukuwa ardhi yao hatua kwa hatua kutoka kwa uongozi wa sasa wa Urusi.

Hata hivyo taarifa hiyo haikuweza kuthibitishwa kwa njia huru. Maafisa wa Urusi pia hawakutoa tamko la haraka kuhusu madai hayo.

Urusi iliyataja makundi ya wapiganaji wa Urusi kuwa vibaraka wa Ukraine

Katika siku za nyuma, maafisa wa Urusi waliyataja makundi hayo kuwa vibaraka vya jeshi la Ukraine na idara kuu ya ujasusi ya Marekani ambayo kwasasa Urusi inadai kuwa inataka kusababisha vurugu nchini humo.

Msemaji wa jeshi la Ukraine Andriy Yusov, ameliambia shirika la habari la 24 Channel nchini humo kwamba makundi hayo yalikuwa yanafanya operesheni zao katika ardhi ya Urusi bila muingilio wa Ukraine.

Soma pia:Zelensky: Dhamira ya kisiasa inahitajika kuisaidia Ukraine

Yusov amesema kundi la tatu la wapiganaji wa kujitolea wa Urusi, pia linashiriki katika operesheni hiyo.

Awali, makundi hayo yalidai kuhusika katika mashambulizi mengine yalioelekezwa nchini Urusi.

Ukraine yafanya mashambulizi nchini Urusi

Ukraine imefanya mashambulizi ya usiku kucha ya zaidi ya droni 25 kuelekea Urusi huku moto ukizuka katika ghala mbili za mafuta na baadhi ya droni hizo kufika ndani ya ardhi ya Urusi. Haya yamesemwa leo na maafisa wa Urusi.

Kiongozi wa kanisa Katoliki dunia Papa Francis katika kikao cha kila wiki cha umma mjini Vatican mnamo Juni 7, 2023
Kiongozi wa kanisa Katoliki dunia Papa FrancisPicha: Ettore Ferrari/ANSA/picture alliance

Wizara ya ulinzi ya Urusi, imesema imeharibu droni 25 ikiwa ni pamoja na mbili katika eneo la Moscow, moja katika eneo la Kaskazini la Leningrad, na 22 katika maeneo ya mpakani ya Belgorod na Kursk, na la mwisho katika eneo la Bryansk.

Kulingana na ripoti za awali, hakuna aliyeathirika kutokana na mashambulizi hayo.

Wizara ya mambo ya nje ya Ukraine yamuita balozi wa Vatican nchini humo

Katika hatua nyingine, wizara ya mambo ya nje ya Ukraine, jana ilimuita balozi wa Vatican nchini humo kuelezea kutoridhishwa kwake na matamshi ya awali yapapa Francis kwamba Ukraine inapaswa kuonesha ujasiri wa kupeperusha bendera nyeupe na kuanza mazungumzo na Urusi ili kumaliza vita vya miaka miwili nchini humo.

Vatican inashinikiza mazungumzo kati ya Urusi na Ukraine

Katika mahojiano na gazeti la Corriere della Sera, naibu wa papa Francis, Kadinali Parolin, amesema kuwa Vatican inashinikiza usitishaji wa mapigano na kwanza ni mchokozi anayepaswa kukomesha mashambulizi.

Soma pia: Ukraine na viongozi wa Magharibi wamkosoa Papa

Matamshi ya papa Francis aliyotoa kama sehemu ya mahojiano aliyofanya mwezi uliopita na kuchapishwa siku ya Jumamosi, yaliibua maoni tofauti kutoka jumuiya ya kujihami ya NATO na Urusi.