1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Majeshi ya Ethiopia, kuondoka Somalia ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Halima Nyanza28 Novemba 2008

Mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia Ahmedou Ould Abdallah amesema umoja huo unapaswa kufanya mazungumzo ya haraka na Ethiopia, ambayo imetangaza kujiondoa kwa majeshi yake ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

https://p.dw.com/p/G5TQ
Miongoni mwa wanajeshi wa Ethiopia, walio katika mji wa Kismayu nchini Somalia.Picha: AP

Mjumbe huyo, Ahmedou Ould Abdallah amesema wasiwasi ulio kwa wote ni kupatikana kwa utulivu nchini Somalia, hivyo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Umoja wa Afrika na Umoja wa Ulaya, unapaswa kujadili suala la kujiondoa kwa majeshi hayo ya Ethiopia.

Ethiopia imetangaza leo kwamba majeshi yake yatajitoa nchini Somalia, ifikapo mwishoni mwa mwaka huu wa 2008, ikiwa ni miaka miwili toka kuingia nchini humo.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje wa Ethiopia Wahide Belay amesema muda huo wa mwisho wa kuondoka ulitangazwa katika barua iliyotumwa siku ya Jumanne kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon pamoja na kwa mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Jean Ping.

Ameeleza kuwa wanajitoa baada ya kufanya kazi waliyoiendea na kwamba wanajivunia kwa hilo, licha ya kwamba hawakufikia matarajio yaliyotegemewa.

Mwanadiplomasia walioiona barua hiyo wamethibitisha uondokaji wa wanajeshi hao wa Ethiopia wanaokadiriwa kufikia elfu 3 utakamilika ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tume ya Afrika Jean Ping, amesema kujiondoa haraka kwa Ethiopia nchini humo, kutaleta matokeo mabaya.

Aidha ameelezea kuwa iwapo hakutakuwa na maelewano ya amani katika serikali hiyo ya mpito, Jeshi la kulinda amani la Umoja wa Afrika limetishia pia kujitoa.

Ethiopia ilituma wanajeshi wake nchini Somalia, mwaka 2006, kuondoa chama kinachojiita Muungano wa Mahakama za Kiislamu ICU, chenye msimamo mkali, ambacho kilikuwa kimetwaa kwa nguvu, maeneo mengi ya nchi hiyo.

Majeshi ya Ethiopia yalipelekwa Somalia kwa ajili ya kuimarisha serikali ya mpito ambayo inapigwa vita na upinzani nchini humo.

Makubaliano ya hivi karibuni kati ya serikali ya mpito ya Somalia na upinzani nchini humo, yalifikia uamuzi wa kuondoka kidogo kidogo kwa majeshi hayo ya Ethiopia, lakini muda wa mwisho kuondoka kwa majeshi hayo haukuwa umetangazwa.

Katika miezi ya hivi karibuni, Ethiopia imekuwa ikisisitiza kwamba haina mpango wa kukaa nchini Somalia, lakini pia imeonya kwamba itarudi tena nchini humo wakati makundi hayo ya waasi yatakaposhika madaraka.

Mwaka uliopita Umoja wa Afrika ulianza kusambaza wanajeshi wa kulinda amani, katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu, lakini majeshi yake yalishindwa kuzuia mapigano yanayoendelea kila siku nchini humu, ambayo yamesababisha vifo vya maelfu ya raia katika kipindi cha mwaka huu pekeee.

Jeshi la Burundi ambalo liko chini ya Kikosi cha Jeshi cha Kulinda amani cha Umioja wa Afrika tayari kimeanza kushika nafasi zilizokuwa zikishikiliwa na Jeshi la Ethiopia katika mji mkuu wa Mogadishu wakati ambao kundi la

Shabab likikaribia mji huo, baada ya kutwaa maeneo mengi.

Kundi la Shabab lililokuwa tawi la kijeshi na la vijana, katika Muungano huo wa Mahakama za Kislamu limekuwa likifanya mashambulio dhidi ya serikali hiyo ya mpito na majeshi hayo ya Ethiopia.

Wachunguzi wa Mambo wanaona kuwa halim iliyop sasa nchini humo inatoa uwezekani mkubwa kwa kundi hilo la Shabab kudhibiti maeneo yote.