Kujizulu kwa Wulff kwamweka matatani Merkel
19 Februari 2012Merkel alilazimika kufuta ziara yake mjini Rome kwa mazungumzo na waziri mkuu wa Italia, Mario Monti, jana Ijumaa wakati taarifa ziliposambaa kuwa Wulff anapanga kujiuzulu, katika muda wa chini ya miaka miwili tangu kuingia madarakani kutokana na shutuma za mahusiano ya karibu na wafanyabiashara tajiri, safari za takrima na mialiko ya kwenda mapumzikoni.
Haya yamejiri baada ya waendesha mashtaka katika jimbo la Lower Saxony nchini Ujerumani kutangaza siku ya Alhamis kuwa wanalitaka bunge la taifa kuondoa uwezo wa kutoweza kushtakiwa kwa kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 52.
Wulff ambaye si mwenye mvuto mkubwa kisiasa, wakati fulani alionekana kuwa mshindani wa Merkel wakati alipokuwa akijisogeza kwenda ngazi za juu katika chama cha Christian Democratic Union, CDU, katika miaka ya 1990.
Baada ya mwanzo mbaya katika kuushughulikia mzozo wa madeni, hisia nchini Ujerumani kuwa Merkel huenda sasa amepoteza mwelekeo katika kulishughulikia suala la mzozo wa kifedha katika bara la Ulaya zilikuwa na maana kuwa maoni ya wapiga kura kumhusu yeye yalifikia kiwango cha juu cha asilimia 64.
Zaidi ya hapo wanauchumi wanasema kuwa kujiuzulu kwa Wulff hakutakuwa na athari yoyote ya moja kwa moja katika hatua za kutanzua mzozo wa madeni na mazungumzo nchini Ugiriki.
Hata hivyo mchumi katika benki ya ING Carsten Brzeski, amesema kuwa mbinyo katika siasa za ndani dhidi ya Angela Merkel unaweza kuongezeka tena na hautaifanya hali yake kuwa na utulivu.
Kwa kuwa hii ni mara ya pili katika muda wa kiasi miaka miwili ambapo Merkel amelazimika kukubali kujiuzulu kwa mtu ambaye amemteua binafsi kushika wadhifa huo wa rais, wadhifa ambao unatakiwa kusaidia kuliweka taifa katika maadili mazuri.
Mei mwaka 2010, Horst Koeler, kiongozi wa zamani wa shirika la fedha la kimataifa, IMF, alijiuzulu kutoka wadhifa huo baada ya matamshi yaliyokuwa na utata aliyoyatoa akishauri kuwa ujumbe wa kijeshi wa Ujerumani katika mataifa ya nje unaweza kutumika kuhimiza masuala ya kibiashara.
Angela Merkel amesema kuwa vyama vinavyounda serikali ya mseto nchini Ujerumani vitafanya mazungumzo na vyama vya upinzani vya Social Democratic, SPD na kile cha Kijani, ili kumtafuta mrithi wa Wulff. Serikali ya mseto ya vyama vya Christian Democratic Union, CDU na Christian Social Union, CSU, pamoja na chama cha kiliberali cha FDP, inataka kufanya mazungumzo yenye lengo la kumpata mgombea wa wadhifa huo atakayekubalika na pande zote. Mwenyekiti wa chama cha SPD, Sigmar Gabriel, amesema yuko tayari kushiriki katika mazungumzo ya haraka yasiyo na masharti. Chama cha kijani pia kimekubali kushiriki katika mazungumzo hayo. Mwenyekiti wa chama cha FDP, Philip Rösler amesema mashauriano yatafanyika kwanza kati ya vyama vilivyomo ndani ya serikali ya mseto kabla ya kuzungumza na vyama vingine.
Hata hivyo kiongozi wa chama cha SPD, Sigmar Gabriel, amesema kuwa chama hicho kiko tayari kwa mwanzo mpya, na kuongeza kuwa ni bora Merkel kuacha kupanga kumpata mgombea anayemtaka yeye kabla ya kukutana na upinzani. Mkuu wa chama cha kijani, Cem Özdemir, amesema kuwa lengo lazima liwe kumpata mgombea ambaye anaungwa mkono na watu wengi.
Mwandishi : Sekione Kitojo / ZR/ dpae
Mhariri: Josephat Charo