Kufungwa kwa Al Jazeera haikubaliki
30 Juni 2017Kufungwa kwa kituo hicho ni mojawapo ya madai 13 yaliowekewa serikali ya Qatar na Saudi Arabia na washirika wake kama adhabu ili nchi hizo ziiondelee vikwazo ilioiwekea nchi hiyo kwa takriban mwezi mmoja sasa.
Nchi hizo nne zimeipa Qatar siku 10 kutekeleza masharti hayo ambayo muda wake wa mwisho unamalizika Julai nne.
Mkuu wa haki za binaadamu wa Umoja wa Mataifa Zeid Raa'd Al Hussein ana wasi wasi mkubwa sana na madai kwamba Qatar ikifunge kituo cha Al-Jazeera na vyombo vyengine vya habari vinavyohusiana navyo hayo yamebainishwa na msemaji wake Ruper Colvile alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Ijumaa.
Ni jambo lisilokubalika
Colvile amesema "Aidha au la umeiangalia,umeipenda au kukubaliana na misimamo yao ya uhariri , matangazo ya Al Jazeera ya lugha ya Kiarabu na Kingereza ni halali na yana watamazaji wengi kwa mamilioni .Madai kwamba yafungwe mara moja kwa maoni yetu ni shambulio lilisokubalika kwa uhuru wa kujieleza na kutowa maoni."
Colvile amesisitiza kwamba nchi zenye kuchukulia vitu kwa kuzingatia mada zinazontagazwa na matangazo ya vituo vya televisheni vya nchi nyengine zina uhuru wa kujadili hadharani na kupinga.
Amesisitiza kwamba ikiwa vituo hivyo vitafungwa litakuwa ni jambo lisilo la kawaida na lisilo kifani na ni wazi kwamba halina msingi.
Marekani itimize dhima muhimu
Kwa kuungwa mkono na Umoja wa Falme za Kiarabu,Misri na Bahrain Wasaudi walitangaza hapo Juni tano wanavunja uhusinao wote ule na Qatar kwa kuishutumu kuunga mkono ugaidi madai ambayo yamekanushwa na serikali ya Qatar.
Ijumaa (30.06.2017)i nchi hiyo imetowa wito kwa mshirika wake Marekani kutimiza dhima muhimu katika kuutatuwa mzozo huo unaozidi kupamba moto kati ya taifa hilo na majirani zake.
Waziri wa mambo ya nje wa Qatar Mohammed bin Abdulraham Al-Thani amesema dhima ya Marekani ni muhimum kwa kuwa wahusika wote katika mzozo huo ni washirika wa serikali ya Marekani.
Kuwait nchi nyengine ya Ghuba imekuwa ikijishughulisha kama mpatanishi kuutatuwa mzozo huo ambao ni mmojawapo wa mzozo mbaya kabisa kuwahi kushuhudiwa katika eneo hili miaka ya hivi karibuni.
Mwandishi : Mohamed Dahman/Reuters /dpa
Mhariri :Yusuf Saumu