1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Korea kaskazini yafunga maeneo zaidi ya mradi wake wa nuklea.

Mohammed Abdul-Rahman18 Julai 2007

Mazungumzo ya awamuya pili ya mkataba uliofikiwa na mataifa sita yanayohusika na mgogoro huo, yanaanza tena leo mjini Beijing.

https://p.dw.com/p/CHAr
Mkuu wa Shirika la nguvu za atomiki la umoja wa mataifa, Mohamed El-Baradei aliyethibisha hatua hiyo ya Korea kaskazini
Mkuu wa Shirika la nguvu za atomiki la umoja wa mataifa, Mohamed El-Baradei aliyethibisha hatua hiyo ya Korea kaskaziniPicha: AP

Mkuu wa shirika la nguvu za atomiki la umoja wa mataifa Dr Mohamed El-Baradei, alisema kwamba wakaguzi wake wamethibitisha kwamba maeneo mengine manne yanayohusiana na madini ya plutonium yamefungwa, hatua inayofuatia kufungwa kwa kinu kikubwa cha Yongbyon Jumamosi iliopita.

Akizungumza na waandishi habari nchini Malaysia Bw El-Baradei alisema sasa kuna hakikisho kwamba maeneo yote matano ya kinuklea yamefungwa.

Kufungwa huko ni hatua ya kwanza kulingana na mkataba uliosainiwa na mataifa sita mwezi Februari, ambapo Korea kaskazini ilikubali hatimae kuachana na mpango wake wa kinuklea, na badala yake kupewa mlolongo wa tija za kiuchumi , kidiplomasia na usalama.

Wakati sasa Korea kaskazini ikiwa imechukua hatua hiyo, wajumbe wa mataifa sita wanaokutana leo mjini Beijing walisema kwamba mazungumzo ya wiki hii hayana budi kuishawishi Korea kaskazini itangaze bayana mipango yake yote ya kinuklea pamoja na kuhakikisha inakon´golewa.

Wajumbe hao ni kutoka China, Korea kaskazini, Korea kusini, Marekani, Urusi na Japan na walikua na milolongo ya mikutano leo asubuhi, kabla ya kuingia katika majadiliano rasmi alasiri. Kabla ya kuanza mkutano wao wa siku mbili mjumbe wa Marekani Christopher Hill alisema wanataka kuhakikisha awamu ya pili inamaliza kazi ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Baada ya mazungumzo yake marefu na mwenzake wa Korea kaskazini Kim Kye-Gam, katika mji mkuu wa China jana, Bw Hill alisema anaamini maendeleo makubwa yatapatikana juma hili.

Lakini Bw Hill pamoja na wajumbe wengine wameungama kwamba bado kuna vikwazo vikubwa vinavyopaswa kukiukwa kabla Korea kaskazini haijafikia hatua ya kutangaza kwamba imeuko´ngoa mradi wake wa nuklea. Mkurugenzi mkuu wa shirika la atomiki la umoja wa mataifa Bw Elbaradei pia leo alizungumzia juu ya matatizo ambayo bado yapo na akaitaka Korea kaskazini ifunguwe milango kuwa ya uwazi zaidi katika hatua hiyo ya kuachana na mpango huo wa silaha za nuklea.

Suala moja kubwa katika awamu hii ya pili ya mkataba uliofikiwa ni amadai ya kuwepo kwa mradi wa siri wa Korea kaskazini kurutubisha madini ya Uranium.

Mazungumzo ya pande hizo sita yalianza 2003, lakini Korea kaskazini ikaendelea kufanya jaribio lake la kwanza la atomiki oktoba mwaka jana, na kusababisha umoja wa mataifa kuiwekea vikwazo. Pyongyang ikajitoa katika mazungumzo hayo na ikarejea baada ya shinikizo kubwa la China , mshirika wae wa karibu , ikiahidiwa tija kubwa ikiwa itaachana na mpango huo wa nuklea moja kwa moja.