Kampuni ya mafuta Trafigura kutoa fidia kwa wahanga wa sumu.
21 Septemba 2009ABIDJAN:
Kampuni ya mafuta Trafigura imekubali kuwalipa fidia watu alfu 31 walioathiriwa na mabaki ya sumu yaliyotupwa nchini Ivory Coast.Na kwa ajili hiyo kampuni hiyo itatoa Euro milioni 30.Msemaji wake amefahamisha kuwa kila mtu atalipwa kiasi cha Euro alfu moja.
Mapatano hayo yalifikiwa nje ya mahakama
Hatahivyo kampuni hiyo ya mafuta imedai kuwa makubaliano hayo hayahusiani na athari za mabaki ya sumu zilizosababisha vifo, magonjwa na kuharibika kwa ujauzito kama ilivyodaiwa hapo awali. Mnamo mwaka wa 2006 ,kampuni ya Trafigura ilikodisha meli iliyosafirisha mabaki ya sumu kutoka Ulaya na kuyatupa pembeni mwa Abidjan, mji mkuu wa Ivory Coast. Serikali ya nchi hiyo imesema watu 17 wamekufa na wengine wasiopungua alfu mia moja wameathirika kutokana na mabaki hayo.