1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kabul. Taliban wadai kumuua mateka wa pili.

31 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CB2J
Baadhi ya jamaa na ndugu wa mateka wa Korea ya kusini , wakisoma ujumbe wa kuomba msaada.
Baadhi ya jamaa na ndugu wa mateka wa Korea ya kusini , wakisoma ujumbe wa kuomba msaada.Picha: AP

Nchini Afghanistan , wapiganaji wa Taliban wanaowashikilia mateka Wakorea ya kusini 22 , wanadai kuwa wamemuua mateka wa pili baada ya muda mwingine wa mwisho uliowekwa kumalizika jana.

Hakuna udhibitisho huru uliotolewa kuwa mateka huyo , mwanamume ameuwawa. Mateka wa kwanza aliuwawa siku tano zilizopita.

Hapo awali , iliripotiwa kuwa wateka nyara hao , ambao wanadai kuachiliwa huru kwa idadi sawa na mateka wao kwa wapiganaji wa Kiislamu, waliweka muda mwingine mpya ifikapo Jumatano.

Wakati huo huo mhandisi wa Kijerumani aliyetekwa nyara na kundi la Taliban siku moja kabla ya kukamatwa kwa Wakorea hao , pia ameendelea kuwa mikononi mwa watekaji nyara hao.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Afghanistan Rangin Spanta hata hivyo amesema kuwa juhudi zinaendelea kupata kuachiwa huru kwa mateka hao.

Tunajitahidi kwa sasa kwa nguvu zetu zote kuwaokoa watu hawa, ikiwa ni suala muhimu kwa sasa. Maafisa, viongozi wa kikabila pamoja na viongozi wa kidini wote wanafanyakazi pamoja na wawakilishi kutoka Korea ili kuwaokoa mateka hao.

Wakati huo huo wizara ya mambo ya ndani imesema kuwa walinzi wa usalama 13 wameuwawa na majeshi ya Taliban katika shambulio la kushtukiza katika barabara kuu ya Kabul hadi Kandahar siku ya Jumapili.