Hali inatisha
21 Septemba 2015Rais Macky Sall wa Senegal,ambae pia ni mwenyekiti wa jumuia ya ushirikiano wa kiuchumi Afrika Magharibi-ECOWAS amesema mbele ya waandishi habari mwisho mwa mazungumzo yao ya upatanishi mjini Ouagadougou,mapendekezo hayo atayafikisha mbele ya viongozi wa ECOWAS watakakaokutana kwa dharura hapo kesho nchini Nigeria.
Mapendekezo hayo yanazungumzia kuhusu kurejeshwa madarakani viongozi wa serikali ya mpito wakiongozwa na rais Michel Kafando,kurejea kambini wanajeshi,kuachiwa huru mateka,kuanza upya maandalizi ya uchaguzi ambao utabidi uitishwe novemba 22 .Mapendekezo hayo yanataja pia uwezekano kwa wafuasi wa rais wa zamani aliyeng'olewa baada ya miaka 27 madarakani Blaise Compaore,kuruhusiwa kugombea uchaguzi huo.Mada hii ndiyo kiini cha madai ya wanajeshi na wafuasi wa Blaise Compaore ambao walipigwa marufuku hapo awali kugombea uchaguzi uliokuwa umepangwa hapo awali kuitishwa october 11.
Hadi wakati huu lakini wapatanishi hao hawakufanikiwa katika juhudi zao za kutaka warejee madarakani viongozi wa serikali ya mpito.
Na hakuna uhakika pia kama mapendekezo hayo ambayo hayakutiwa saini,yataungwa mkono na wanajeshi waliofanya mapinduzi,waliokuwa wamemkamata rais wa mpito,waziri mkuu na mawaziri wake wawili , wapinzani wao wa kisiasa au mashirika ya kijamii.
Mmojawapo wa wawakilishi wa serikali ya mpito,mazungumzoni anasema:
"Tutapambana.Nchini Burkina faso tuna usemi,bora kufa wima kuliko kuwa hai na kupakata mikono.Wanasema tumekubali,tumekubali nini?Hatujakubali chochote.Tunahisi huu ni usaliti,kutoka kwa rais Macky Sall na pia jumuia ya uchumi ya ECOWAS."
Wawakilishi wa kikosi maalum cha ulinzi wa rais kinachoongozwa na kiongozi wa mapinduzi Gilbert Diendéré-mshirika mkubwa wa rais wa zamani Blaise Compaore wanasema watayadurusu mapendekezo hayo.
Akiwa ziarani nchini Marokko,rais Francois Hollande wa Ufaransa mtawala wa zamani wa kikoloni amewatolea wito waburkinabe waunge mkono juhudi za upatanishi na kuwaonya wale wanaozipinga juhudi hizo.
Hali bado ni tete nchini Burkina fasio ambako sheria ya kutrotoka nje usiku bado inaendelea.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP/dpa
Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman