1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Johnson kwenda Brussels kwa mazungumzo zaidi ya Brexit

Lilian Mtono
8 Desemba 2020

Waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson anatarajiwa kwenda Brussels kwa ajili ya majadiliano ya kina baada ya mazungumzo ya muda mrefu ya simu na rais wa Halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen.

https://p.dw.com/p/3mNhr
Johnson stimmt Großbritannien auf harten Bruch mit EU ein
Picha: Downing Street/PA/dpa/picture-alliance

Hata hivyo wakuu hao wawili wanakiri kwamba bado kuna tofauti baina yao. 

Taarifa ya pamoja kutoka kwa waziri mkuu wa Uingereza Boris Johnson na rais wa halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen hapo jana Jumatatu imesema kwamba masharti ya makubaliano bado hayajafikiwa.

Taarifa hiyo imesema walikubaliana kwamba masharti ya kukamilisha makubaliano hayakuwepo kwa sababu ya tofauti kubwa iliyobaki juu ya maswala matatu muhimu ya mazingira ya usawa kwenye ushindani wa kibiashara, makubaliano ya masuala ya uvuvi na usimamizi na uendeshaji wa mambo hayo.

Taarifa hiyo ilisema wamewaomba wawakilishi kwenye mazungumzo hayo kuandaa muhtasari kuhusiana na tofauti hizo zilizosalia na zinazotakiwa kujadiliwa kwenye mkutano utakaowakutanisha ana kwa ana mjini Brussels katika siku zijazo.

Johnson na von der Leyen waliripotiwa kufanya mazungumzo ya simu kwa takriban saa moja na nusu jana Jumatatu kabla ya kukubaliana kupumzika na saa moja baadae kukatolewa taarifa hiyo.

Wakuu hao wawili walizungumza kwanza siku ya Jumamosi lakini walikiri kwamba bado kunasalia tofauti kubwaUmoja wa Ulaya, Uingereza zarejea kwenye meza ya mazungumzo

Irland, Dublin:  'Getting Ireland Brexit Ready' Workshop
Waziri wa mabo ya kigeni wa Ireland Simon Coveney aonya kuhusu matarajio hasi juu ya mazungumzo hayo.Picha: Reuters/C. Kilcoyne

Ireland yaonya kuhusu "matarajio hasi".

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ireland Simon Coveney ameonya kuhusu kuongezeka matarajio hasi kwamba timu zinazofanya mazungumzo zinaweza kufanikisha makubaliano mchakato huo bila ya kuingiliwa na Johnson na von der Leyen. Coveney amesema alipowasili Dublin akitokea Brussels kwamba siku mbili zijazo zina umuhimu mkubwa kuliko siku mbili zilizopita na kuongeza kuwa kuna sintofahamu kubwa sio tu kwa wawakilishi wa mazungumzo hayo, bali pia mataifa wanachama.

Alisema "Tuko katika wakati muhimu sana wa makubaliano. Na bila ya uingiliaji wa kisiasa kutoka juu, nikimaanisha kwa waziri mkuu na rais basi nadhani kwamba watu wananazidi kuwa na matarajio hasi kwamba timu za mazungumzo zinaweza kumaliza hili kwa mafanikio. Tuna siku mbili za mazungumzo ya kina baada ya mapumziko.... Na kwa kweli hakukua na hatua yoyote iliyopigwa, kwa siku hizo mbili, kwa bahati mbaya."

Serikali ya Uingereza ilisema Jumatatu mchana kwamba ilikuwa tayari kuvunja vifungu vya sheria ya Brexit ambavyo vitairuhusu pia kuvunja sheria ya kimataifa linapokuja suala la taratibu za forodha kwa bidhaa zinazotoka Ireland Kaskazini. 

Jana jioni, wabunge 357 wa Uingereza waliupigia kura muswada wenye utata juu ya Masoko ya Ndani, unaoanzisha sheria ya kuratibu biashara miongoni mwa mataifa manne yanayounda Ufalme wa Uingereza, baada ya kujitoa kwenye Umoja wa Ulaya, dhidi ya 268 walioupinga.

Hata kama makubaliano yakifikiwa, uwezekano wa kuhitimisha rasmi mchakato huo kabla ya mwisho wa mwaka, wakati ukomo uliowekwa wa muda wa Uingereza kujiondoa nao ukikamilika tayari unaonekana ni finyu mno.

Soma Zaidi: Uingereza haitabadilisha msimamo kuhusu Brexit

Mashirika: DW/AFPE