1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jenerali Musharraf aanza kuviaga vikosi vya jeshi

27 Novemba 2007
https://p.dw.com/p/CTXh

Rais Pervez Musharraf wa Pakistan leo anaanza ziara za kuviaga vikosi vyake, siku moja kabla kujiuzulu wadhifa wa mkuu wa majeshi na kuapishwa kuwa rais wa kiraia.

Kiongozi huyo atawacha wadhifa wake jeshini hapo kesho na kuapishwa kuwa rais wa kiraia hapo keshokutwa.

Jenerali Musharraf atayatembelea makao makuu ya kikosi cha pamoja, jeshi la maji na jeshi la anga, yaliyo kati ya mji mkuu Islamabad na mji wa Rawalpindi.

Hapo kesho rais Musharraf atakwenda katika makao makuu ya mkuu wa majeshi mjini Rawalpindi, ambako atajiuzulu rasmi na kukabidhi wadhifa wake kwa jenerali Ashfaq Kiyani.

Kiongozi huyo atafanyiwa gwaride ya heshima wakati atakapokabidhi wadhifa wake.