1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran yafanyia majaribio makombora yake tisa.

Nyanza, Halima9 Julai 2008

Iran leo imefanya majaribio ya makombora yake, ambayo masafa yake yanaifikia Israel, hali ambayo imeiudhi Marekani.

https://p.dw.com/p/EZ7i
Rais wa Iran Mahmoud Ahmadinejad, aliyeko kati, pamoja na maafisa wake wakiwa wameizunguuka roketi ya utafiti iliyozinduliwa hivi karibuni. Iran pia leo imefanyia majaribio makombora yake tisa.Picha: AP

Kombora chapa Shahab 3, ni miongoni mwa makombora tisa yaliyofanyiwa majaribio hayo ya mashambulio, mapema leo asubuhi kutoka katika eneo lisilojulikana kwenye jangwa la nchi hiyo.

Kwa mujibu wa kituo cha televisheni cha serikali ya nchi hiyo Al Alam, makombora hayo yaliyofanyiwa majaribio na kikosi maalumu cha jeshi, likiwemo hilo la Shahab 3 lenye uzito wa tani moja na linalokwenda masafa ya kilomita elfu 2.

Jaribio hilo la makombora limefanywa wakati hofu ikiongezeka juu ya mradi wa nyuklia wa Iran, ambapo nchi hiyo imekuwa ikisisitiza ni mradi huo ni wa amani, kwa ajili ya matumizi ya kawaida kutokana na ongezeko la idadi ya watu nchini humo, lakini hata hivyo nchi za magharibi zinahofia kuwa mradi huo unalengo la kutengeneza silaha za nyuklia.

Kamanda wa Kikosi cha Anga nchini humo, Hossein Salami amenukuliwa na televisheni ya serikali ya nchi akisema azma ya zoezi hilo la kijeshi, ni kuonesha kuwa wako tayari kulinda mamlaka ya dola la Iran.

Amesema makombora yao yako tayari kushambulia eneo lolote, wakati wowote kwa haraka na usahihi na kuongeza kusema kuwa maadui wao wasirudie makosa yao kwani shabaha za maadui wao zinachunguzwa.

Marekani ambayo haikuondoa uwezekeano wa kuishambulia Iran, imelaani haraka jaribio hilo la makombora lililofanywa na nchi hiyo.

Msemaji wa Ikulu ya Marekani Gordon Johndroe amesema hatua za Iran kuendelea na makombora haya zinakwenda kinyume na maazimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa na inakwenda kinyume na wajibu wa Iran katika dunia.

Mbali na kombora chapa Shahab 3, ambalo ni miongoni mwa makombora tisa yaliyofanyiwa majaribio mengine ni Zelzal linalokwenda masafa ya kilometa hadi 400 na Fateh linalokwenda kilomita 170.

Iran ilifanya jaribio la kombora lake hilo la Shahab 3 kwa mara ya kwanza, katika zoezi lililofanyika Novemba 2006.

Katika hatua nyingine Naibu Mkuu wa Shirika la Iran la Nishati ya Nyuklia Mohammad Saeedi amesema nchi yake inatarajia kufanya mazungumzo katika siku chache zijazo kuhusiana na mzozo wa mradi wake wa nyuklia.

Amesema ni jambo zuri kutokana na nchi za magharibi kukubali kuanza majadiliano na Iran juu ya suala hilo.