Interpol yaombwa msaada kumkamata Ben Ali
26 Januari 2011Shirika la Interpol limeombwa kutoa waranti ya kumkamata Ben Ali, mkewe Leila Trabelsi na jamaa zao, kwa mashtaka ya kupora mali ya taifa na kuhamisha fedha za kigeni katika nchi za ngámbo. Hayo alitamka Waziri wa sheria wa Tunisia, Lazhar Karoui Chebbi alipokutana na waandishi wa habari mjini Tunis hii leo. Waziri huyo akaongezea kuwa watu saba walio jamaa wa Ben Ali wamezuiliwa Tunis,lakini mpwa wa mkewe, Imed Trebelsi na mkwe wa Ben Ali, Sakher al-Materi wamekimbilia nchi za ngámbo.
Familia na jamaa za Ben Ali na hasa ukoo wa Trabelsi wanatuhumiwa kuwa walitumia uhusiano wao wa kisiasa kujirundikia mali. Sasa, serikali inataka msaada wa Interpol kumkamata Ben Ali, mkewe na wengine waliotoroka, ili wapate kufikishwa mahakamani nchini Tunisia. Ben Ali alijikusanyia mali wakati wa utawala wake wa miaka 23 na familia yake ilidhibiti makampuni mengi makubwa nchini humo. Ombi la Tunisia kwa Interpol limetolewa wakati wananchi wakiingojea serikali kutangaza mageuzi katika serikali ya mpito.
Hatua hiyo inachukuliwa kuitikia mito ya wananchi wanaoendelea kuandamana, wakipinga kuteuliwa kwa mawaziri kadhaa walioitumikia serikali ya zamani ya Ben Ali, akiwemo pia Waziri Mkuu Mohammed Ghannouchi. Leo, polisi walitumia mabomu ya kutoa machozi, kuwatawanya kiasi ya waandamanaji 1,000 waliokusanyika nje ya ofisi ya Ghannouchi tangu siku ya Jumapili. Ben Ali alikimbilia Saudi Arabia Januari 14, kufuatia maandamano ya mwezi mzima yaliyosababisha vifo vya watu dazeni kadhaa.
Mwandishi:P.Martin/DPAE/RTRE
Mpitiaji: Abdul-Rahman,Mohammed