1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hoffenheim waipiku B.Munich

15 Desemba 2008

Hoffenheim iliopanda daraja ya kwanza imeibuka kileleni mwa Bundesliga na mabingwa wa nusu msimu.

https://p.dw.com/p/GGZV
Hoffenheim washangiriaPicha: AP

Hoffenheim imewapiku mabingwa watetezi Bayern Munich jana na kutawazwa wao mabingwa wa duru ya kwanza ya msimu wa Bundesliga-

Kocha wa Chelsea -mbrazil Luiz Felipe Scolari amefadhahishwa kwanini Chelsea yashindwa kutamba nyumbani-FC barcelona na Samuel Eto-o watamba mbele ya mabingwa Real Madrid katika La Liga na katika kinyanganyiro cha kombe la klabu bingwa za dunia huko Tokyo,Japan,Adelaide United ya Australia imetimua Gamba Osaka ya Japan kwa bao 1:0 na ina miadi sasa na mabingwa wa Afrika Al Ahly. Taifa Stars,yakata tiketi za kombe la Afrika mwakani nchini Ivory Coast kwa timu za wachezaji wanaocheza Afrika tu baada ya kuiomea Sudam 2:1.Na

katika ringi ya mabondia,Vitali Klitschko wa Ukraine amekubali kuingia ringi mwakani mjini London na Muingereza David Haye kuania taji la wezani wa juu ulimwenguni.

Tuanze na Ligi mashuhuri barani Ulaya: katika Bundesliga-Ligi ya Ujerumani, klabu iliopanda daraja ya kwanza msimu huu tu ilitawazwa jana mabingwa wa duru ya kwanza ya msimu wa Bundesliga baada ya kutoka nyuma na kusawazisha bao 1:1 na Schalke. Timu hii ya kijijini,imefanya kwahivyo maajabu kwani hakuna alieitazamia kuwa kileleni mwa Bundesliga wakati huu.

Ilikua schalke lakini iliolifumania kwanza lango la Hoffenheim pale mchezaji wa taifa wa asili ya Ghana,Gerald Asamoah,alipoipatia Schalke bao .Halafu mkwaju mkali wa freekicke aliouchapa Selim Teber uliponasa wavuni.

Bayern Munic iliongoza kwa mabao 2 kabla Stuttgart kuwaambia majirani zao wa kusini kwamba "kutangulia si kufika." Khedira alifuta mabao hayo 2 kwa yake 2 na kuondoka suluhu.

Hertha Berlin iliendelea kutamba na kuhakikisha nafasi yake ya 3 nyuma ya Hoffenheim na Bayern Munich.Berlin iliizaba Karlsruhe mabao 4-0 katika Uwanja wa olimpik. Hamburg imeondokea nafasi ya 4 kufuastia ushuindi wao wa bao 1-0 dhidi ya Frankfurt kwavile jogoo lao la croatia Mladen Petric liliwika tena.

Bayer Leverkusen iliokua mwanzo kileleni sasa imeangukia nafasi ya 5.

Kijijini Hoffenheim jana ilikua shangwe na shamra shamra na baadhi ya mashabiki walianza kutabiri mwishoe, Hoffenheim itatoroka na kombe:

"Ndio Hoffeinheim iibuke bingwa." walidai mashabiki hao.Nae kocha wao aliezusha maajabu haya Ralf Ringnick alisema:

"Kuwa msimu ujao hatutashuka daraja ya pili hii sasa ni hakika kabisa.Na hilo ndilo jukumu kubwa tulioipa timu yetu na chochote sasa zaidi kitakachokuja tukipokee."

Tukigeukia Ligi nyengine barani ulaya-changamoto kati ya majogoo wawili wakubwa nchini Spain-mabingwa Real Madrid na Fc Barcelona.Barcelona kwa ushindi wa mabao 2:0 nyumbani mwa Real ,imefungua sasa mwanya wa pointi 12 kati yake na mabingwa.Bao la Mkamerun Samuel Eto na muargentina Lionel Messi yalipiga msumari wa mwisho katika jeneza la Real Madrid.FC Barcelona kwahivyo tayari inashangiria ubingwa nchini Spain na sasa muhimu kwa Barcelona ni kutamba mbele ya valencia na kuingia mwaka mpya bila ya wasi wasi.Katika orodha ya watiaji magoli mengi, mkamerun samuel eto anaongoza kwa mabao yake 15 kwa 12 ya David Villa wa Valencia.

Ama Chelsea imeregeza kamba katika Premier League-Ligi ya Uingereza baada ya kutoweza kwa mara nyengine tena kutamba nyumbani.Chelsea imepoteza nafasi yake mwishoni mwa wiki kuipiku Liverpool na kuparamia kileleni.Ilitoka sare tu bao 1-1 na West ham.Kwa matokeo hayo, Chelsea imebaki nafasi ya pili nyuma ya Liverpool.Kushindwa kutamba nyumbani kumemtia wasi wasi kocha wa Chelsea-mbrazil Luiz Felipe Scolari.Haelewi kwanini Chelsea inatamba nje na inashindwa nyumbani.

Wakati kinyanganyiro cha Ligi barani ulaya kinakaribia kwenda likizoni kwa siku kuu za x-masi na mwaka mpya, klabu bingwa za mabara yote ziko Japan wakati huu kuania taji la klabu bingwa ya dunia:Afrika inawakilishwa na Al Ahly ya Misri ambayo ina miadi na Adelaide kwa mpambano wake ujao.Adelaide ya Australia, ilitamba kwa bao 1-0.

Changamoto kati ya Adelaide United na mabingwa mara 6 wa Afrika-Al Ahly ya Misri itakua alhamisi hii ijayo.Mabingwa hao wa Afrika walizabwa mabao 4-2 na Pachuca ya Mexico katika hatua ya robo-finali.

Mabingwa wa Ulaya Manchester United wanatamani kuwa timu ya kwanza ya Uingereza kutawazwa klabu bingwa ya dunia.Kwani, hilo ni moja kati ya mataji machache ambayo Manchester bado haikuvaa.Manchester iliowasili Tokyo leo ilitoka sare 0:0 juzi jumamosi nyumbani ilipocheza na Tottenham.

Manchester United ilipotawazwa mabingwa wa ulaya 1999 iliania kombe hili lilipochezwa kwa mara ya kwanza kabisa huko Brazil ,lakini Manu haikuvuka robo-finali.Ililazwa kwa mabao 3-1 na Vasco De Gama.

Manchester inaingia moja kwa moja katika hatua ya nusu-finali ya kinyanganyiro hiki cha timu 7 na alhamisi hii ijayo Manu ina miadi na Gamba Osaka ya Japan. Gamba imeiahidi Manchester changamoto kali,kwani imeapa kutoliachia jogoo la shamba kuwika mjini Tokyo.

Tanzania imekata mwishoni mwa wiki tiketi yake ya kushiriki kwa mara ya kwanza katika mashindano makuu ya dimba tangu iliposhiriki huko Nigeria katika All-Africa Games 1973 na kombe la Afrika la mataifa miaka ya 1980.Februari ijayo, Taifa Stars watashiriki katika kombe maalumu la Afrika la wachezaji wasiocheza nchi za ngambo. Ushindi jumamosi wa mabao 2-1 dhidi ya Sudan, ulitosha kuipeperusha Taifa Stars hadi Abidjan,Corte d-Iviore.

Mbabe wa wezani wa juu ulimwenguni, Vitali Klitschko wa Ukraine, amepanga changamoto mwakani kutetea taji lake la wezani wa juu ulimwenguni na Muingereza David Haye, miaka 28.Haye, bingwa wa dunia wa wezani wa cruiserweight,alijitosa katika wezani wa juu ulimwenguni alipomzima Monte Barret katika duru ya 5 mwezi uliopita huko London.

Wladmir Klitschko,nduguye Vitali, ni bingwa wa taji la dunia la wezani wa juu la shirika la IBF na WBO.