GUANGXI:wafanyaghasia kupinga kuzuiwa kuzaa
22 Mei 2007Matangazo
Maelfu ya wanavijiji huko kusini magharibi mwa China wamechoma moto nyumba na kuvunja magari katika ghasia zilizosababishwa na sera ya China kutaka kila familia kutokuwa na mtoto zaidi ya mmoja.
Ghasia hizo zilitokea Ijumaa na Jumamosi, katika jimbo la Guangxi, baada ya maafisa wa serikali kuanza kuzitoza faini au kuchukua mali za familia zenye watoto wengi,
China inaruhusu familia zinazoishi mijini kuwa na mtoto mmoja, ambapo kwa familia za vijijini, zinaruhusiwa kuwa na watoto wawili iwapo mtoto wa kwanza atakuwa ni msichana.
Sheria hiyo ilianzishwa nchini China katika miaka ya sabini, ikiwa ni njia ya kukabiliana na ongezeko kubwa la idadi ya watu katika taifa hilo linaloongoza likiwa na kiasi cha watu billioni 1.3.